2013-12-05 10:57:44

Yesu ni mwamba thabiti, dira na nguzo ya maisha ya waamini inayopaswa kushuhudiwa kwa matendo zaidi!


Waamini wanatakiwa kusikiliza kwa makini, kulitafakari Neno la Mungu na hatimaye, kulimwilisha katika maisha na vipaumbele vyao, kwa kutambua kwamba Yesu Kristo ni mwamba imara wa maisha, kiini na chemchemi ya umoja, upendo na mshikamano wa dhati.

Haitoshi kuzifahamu Amri za Mungu, bali kuzitekeleza na kuzimwilisha katika uhalisia wa maisha ya kila siku. Neno la Mungu ni msingi thabiti ambao waamini wanaweza kujenga maisha yao juu yake, bila wasi wasi wowote!

Ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Ibada ya Misa Takatifu, Alhamisi, tarehe 5 Desemba, 2013 kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican. Anasema, Yesu ni mwamba thabiti na chemchemi ya maisha ya waamini, kiasi kwamba, wanaweza kusonga mbele pasi na mashaka. Neno la Kristo halina budi kumkumbatia Yesu Kristo mwenyewe, vinginevyo kuna hatari kubwa. Waamini hawana budu kuhakikisha kwamba, maneno na matendo yao yanaonesha ile imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, katika unyenyekevu kama alivyofanya Bikira Maria.

Yesu awe ni mwamba, dira na nguzo ya maisha ya waamini si tu kwa maneno bali kwa njia ya ushuhuda wa imani tendaji. Waamini wajenge uhusiano wa karibu zaidi na Kristo kwa njia ya Neno, Sakramenti na Matendo ya huruma, kama kielelezo cha kuwashirikisha wengine upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Waamini wajenge maisha na familia zao katika Mwamba thabiti ambao ni Yesu Kristo Mkombozi wa dunia. Ni changamoto kwa waamini kuchunguza dhamiri zao na kuona ikiwa kama maneno wanayokiri kwa vinywa vyao yanakwenda sanjari na matendo yao ya Kikristo.

Unyenyekevu uwawezeshe waamini kusonga mbele ili kutangaza matendo makuu ya Mungu, vinginevyo, kiburi na majivuno yanaweza kuwasababishia majanga ya kiimani!







All the contents on this site are copyrighted ©.