Watu wanamiminika mjini Vatican ili: kumwona, kumsikiliza na kumwombea Papa Francisko
mtu wa watu!
Sr. Maximilliana Immaculata wa Shirika la Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili kutoka
Tanzania anasema kwamba, amefurahi kushiriki katika Katekesi ya Baba Mtakatifu Francisko,
Jumatano tarehe 4 Desemba 2013 na hivyo kuungana na maelfu ya watu wanaomiminika kila
siku mjini Vatican ili kumwona, kumsikiliza na kumwombea katika maisha na utume wake
kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, wakati huu Kanisa linapoendelea kukabiliana na changamoto
mbali mbali kutoka katika ulimwengu wa utandawazi.
Anasema, alipokuwa
kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican amejisikia kuwa na amani
ya ndani, faraja, imani na nguvu ya kusonga mbele katika maisha na utume wake kama
Mtawa. Mwaka wa Imani uliohitimishwa na Mama Kanisa kwa Sherehe za Kristo Mfalme ni
mwaliko kwa waamini kumtambua Yesu Kristo kuwa ni Mfalme wao wa maisha, Kiongozi wao
mkuu na Mchungaji mwema aliyethubutu kuyamimina maisha yake ili kumkomboa mwanadamu
kutoka katika lindi la dhambi na mauti.
Mwaka wa Imani imekuwa ni fursa kubwa
kwa waamini kuweza kufanya tafakari ya kina kuhusu: Imani wanayoungama na kuikiri
kwa vinywa vyao; Imani wanayoadhimisha katika Liturujia na Sakramenti za Kanisa; Imani
wanaoishi kadiri ya Amri za Mungu, sheria na kanuni maadili; Imani wanayosali katika
Zaburi, lakini zaidi katika Sala mbali mbali za Kanisa na binafsi. Ni mwaliko kwa
waamini kuhifadhi utajiri huu ili kuutolea ushuhuda wa kweli!