2013-12-04 10:40:42

Tuzo ya heshima kwa Papa mstaafu Benedikto XVI kwa kusimama kidete kulinda na kutetea maadili na utu wema katika mambo ya fedha na uchumi!


Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI ametunukiwa tuzo ya heshima kwa kusimama kidete katika kukazia misingi ya maadili na utu wema katika masuala ya fedha na uchumi kwa ajili ya mafao na ustawi wa binadamu na Baraza la Kipapa la haki na amani. Kanuni maadili, utu na heshima ya binadamu ni mambo yanayowaunganisha wasomi, wafanyabiashara na watu wanaojitolea.

Tuzo hii imetolewa wakati wa semina ya kimataifa iliyokuwa imeandaliwa na Baraza la Kipapa la haki na amani, tangu tarehe 2 Desemba hadi tarehe 4 Desemba, 2013. Siku ya Jumatano, tarehe 4 Desemba 2013, wajumbe wamehudhuria Katekesi ya Baba Mtakatifu Francisko kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Tukio hili limehudhuriwa na viongozi waandamizi kutoka Vatican.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita anastahili tuzo hii ya heshima kwa bidii na juhudi alizozionesha wakati Jumuiya ya Kimataifa ilipojikuta imetumbukia kwenye athari za myumbo wa uchumi kimataifa; fursa za ajira zikatoweka, Mabenki yakafilisika na viwanda vikafungwa kutokana na ukata uliosababishwa na ukosefu wa kanuni maadili, utu na heshima ya binadamu; watu wengi katika masuala ya fedha na uchumi walielemewa na uchu wa kutaka kupata faida kubwa, hapa ukawa ni mwanzo wa majanga kwa binadamu!







All the contents on this site are copyrighted ©.