2013-12-04 08:29:01

Mshikamano wa kimataifa unahitajika ili kupambana na baa la njaa na umaskini wa hali na kipato!


Mabadiliko ya tabia nchi ni jambo linalogusa kwa namna ya pekee haki na usawa katika Jumuiya ya Kimataifa. Athari za mabadiliko ya tabianchi zinaonesha kwamba, kuna umuhimu kwa Jumuiya ya Kimataifa kushirikiana na kushikamana katika kuibua mbinu muafaka utakaodhibiti athari za mabadiliko ya tabianchi. RealAudioMP3
Kwanza watu hawana budi kurekebisha mitindo ya maisha ambayo inachangia kwa kiasi kikubwa kuchafuzi wa mazingira, lakini zaidi katika harakati za Jumuiya ya Kimataifa kukabiliana na baa la njaa pamoja na umaskini wa hali na kipato unaoendelea kunyanyasa maisha ya mamillioni ya watu duniani.
Ni mchango wa Askofu mkuu Celestino Migliore Balozi wa Vatican nchini Poland, wakati alipokuwa anachangia hivi karibuni katika mkutano wa mabadiliko ya tabianchi uliokuwa umeandaliwa na Umoja wa Mataifa, mkutano ambao umehitimishwa pasi na mafanikio makubwa, baada ya nchi wanachama kushindwa kuafikiana jinsi ya kugharimia udhibiti wa mabadiliko ya tabianchi kwa kupunguza pia hewa ya ukaa angani.
Askofu mkuu Migliore anasema, kipeumbele cha kwanza hakina budi kutolewa kwa utu na heshima ya binadamu, misingi ya maadili na utu wema, mafao ya wengi; hifadhi na msaada kwa maskini na watu wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii bila kuwasahau vijana ambao ni waathirika wakubwa wa mabadiliko ya tabianchi; kuzingatia na kuenzi haki jamii na usawa. Mambo haya yakizingatiwa na Jumuiya ya Kimataifa kunawezekano kwa Jumuiya ya Kimataifa kufikia muafaka juu ya mikakati inayoweza kutumiwa katika kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.
Jumuiya ya Kimataifa haina budi kujikita katika mchakato wa kulinda na kutunza ukanda wa Ozone; kuangalia kiwango cha maendeleo yaliyofikiwa na nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, ili kwamba, nchi changa zaidi duniani ziweze kusaidiwa ili kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na kuanza kutumia teknolojia rafiki kwa mazingira. Suluhu za kiteknolojia ni muhimu sana, lakini wakati mwingine hazitekelezeki. Jumuiya ya Kimataifa haina budi kuwekeza katika sera ya upashanaji habari na elimu ya mazingita mintarafu kanuni maadili, ili kulinda pia ekolojia ya binadamu.
Athari za mabadiliko ya tabianchi zina uhusiano wa karibu na kumong’onyoka kwa misingi ya maadili, myumbo wa uchumi kimataifa na harakati za kutafuta maendeleo endelevu. Askofu mkuu Migliore anasema, mambo yote haya yanahitaji kwa namna ya pekee uwajibikaji wa pamoja miongoni mwa familia ya binadamu, kwa kutoa kipaumbele cha pekee kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.








All the contents on this site are copyrighted ©.