Kwa njia ya ubatizo, waamini wanashiriki: mateso, kifo na ufufuko wa Kristo!
Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Katekesi yake, kama sehemu ya mwendelezo wa tafakari
ya kina kuhusu Kanuni ya Imani, siku ya Jumatano, tarehe 4 Desemba 2013 amegusia sehemu
ya mwisho ya Kanuni ya Imani isemayo "Nangojea na ufufuko wa wafu na uzima wa milele
ijayo".
Anakiri kwamba, si rahisi kuweza kuifahamu sehemu hii ya Kanuni ya
Imani, lakini Injili inaonesha kwamba, ufufuko wa wafu una uhusiano wa pekee na Ufufuko
wa Yesu Kristo, kielelezo kwamba kuna Ufufuko wa wafu. Baba Mtakatifu amefafanua sehemu
hii ya Kanuni ya Imani kwa kukazia mambo makuu matatu yanayoonesha uhusiano uliopo
kati ya ufufuko wa Kristo na ufufuko wa watu.
Maandiko Matakatifu yanaonesha
hija ya imani kuelekea kwenye ufufuko wa wafu. Ni imani inaomwonesha Mwenyezi Mungu,
aliyemuumba mwanadamu: mwili na roho. Huyu ni Mungu ambaye ni Mkombozi anayewajalia
waja wake Roho Mtakatifu ili aweze kuwaimarisha. Ufufuko wa wafu ni mwanzo wa maisha
mapya ya Waisraeli, walioshindwa vitani na kunyanyasika sana! Yesu katika Agano Jipya
anaonesha ukamilifu wa Imani juu ya Ufufuko wa wafu kwa kuihusisha na maisha yake
binafsi, anaposema kwamba, Yeye ndiye Ufufuko na Uzima. Siku ya mwisho, Yesu atawafufua
wote wanao mwamini.
Baba Mtakatifu anasema, Yesu alifanyika mwili katika mambo
yote akawa sawa na binadamu, isipokuwa hakutenda dhambi, kwa njia hii amewaachia wafuasi
wake njia inayowaelekeza mbinguni kwa Baba yake. Ni Neno wa Mungu aliyefanyika mwili,
aliyeteswa, akafa na kufufuka kwa ajili ya binadamu; ndiye anayewakirimia wafuasi
wake Roho Mtakatifu anayekamilisha umoja na Ufalme wa utukufu na uzima wa milele,
ambao waamini wanausubiri kwa hamu.
Haya ndiyo matumaini yanayomwelekeza mwamini
pamoja na Jumuiya ya waamini mwanga wa matumaini yanayookoa kama anavyosema Baba Mtakatifu
mstaafu Benedikto XVI. Wakristo ni wafuasi wa yule aliyekuja, anayekuja na atakayekuja
nyakati za mwisho, mwaliko wa kutembea katika huruma na kwenye njia ya wokovu.
Baba
Mtakatifu Francisko anasema, ufufuko wa wafu utakuja siku ya mwisho na kwamba, hii
ni kazi inayoonesha nguvu ya Mungu atakayeifufua miili kwa kuipatia tena roho kwa
nguvu ya ufufuko wa Kristo; mageuzi ambayo yanapaswa kufanyiwa kazi na waamini wakati
wanapoishi hapa duniani kwa kukutana na Yesu Mfufuka katika Sakramenti, na hasa Sakramenti
ya Ekaristi Takatifu. Waamini katika hija ya maisha yao hawa ndio wale wanaokula Mwili
na kunywa Damu Azizi ya Yesu, ili hatimaye, kupata maisha ya uzima wa milele. Miili
hii itapata utukufu na maisha ya uzima wa milele
Baba Mtakatifu anawaambia
waamini kwamba, katika maisha yao hapa duniani wanashiriki pia katika Ufufuko wa Kristo,
kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo, inayowashirikisha katika kifo na ufufuko wake ili
kuwashirikisha maisha mapya, yaani ya watu waliofufuka katika Kristo. Kila mtu anashiriki
katika umilele, hivyo anapaswa kuheshimiwa, kupendwa na kuthaminiwa hata katika hali
ya magonjwa, ili waweze kuonja uwepo wa karibu wa Ufalme wa Mungu, ambao tayari wameanza
safari ya kuuendea.
Akizungumza na mahujaji kwa lugha mbali mbali amewataka
mahujaji wanaozungumza Kifaransa kukazia majiundo ya kimissionari kama njia ya kuimarisha
imani katika ufufuko wa wafu! Yesu ni Hema la Mungu, linalopata makazi yake kati ya
watu! Mwaliko kwa waamini kumwendea ili waweze kupata maisha ya uzima wa milele.
Kipindi
cha Majilio ni wakati muafaka wa kutafakari Fumbo la Umwilisho, kielelezo cha upendo
na huruma ya Mungu anayekuja kumkomboa mwanadamu. Waamini wanaalika kukesha kwa njia
ya Sala, Tafakari ya Neno la Mungu pamoja na matendo ya huruma. Bikira Maria ni mfano
bora wa kuigwa katika hija ya kukutana na Yesu anayekuja kati ya watu wake. Kila mwamini
anakumbushwa wajibu wake wa kutangaza Injili kwa njia ya ushuhuda wa maisha, kama
alivyofanya Mtakatifu Francisko Xsaveri.
Mwishoni mwa Katekesi yake, Baba
Mtakatifu Francisko amewaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusali kwa
ajili ya kuwaombea watawa waliotekwa nyara kutoka katika Monasteri ya Waothordox wa
Kigriki ya Mtakatifu Tecla huko Ma'Lula nchini Syria, siku chache zilizopita. Baba
Mtakatifu amewaombea watawa na watu wote ambao wametekwa nyara kutokana na vita inayoendelea
nchini Syria. Kwa pamoja waendelee kusali na kusimama kidete kulinda na kutetea amani.