2013-12-04 10:21:45

Injili ya Furaha ni changamoto na mwaliko wa kufanya toba, wongofu ili kuleta mabadiliko katika maisha na utume wa Kanisa


Dr. Olav Fyske Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni anasema, Waraka wa Kitume Evangelii Gaudium, Injili ya Fuaraha uliochapishwa na Baba Mtakatifu Francisko ni changamoto na mwaliko katika maisha na utume wa Kanisa katika mchakato wa utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia.

Ni waraka ambao umepokelewa kwa mikono miwili na wajumbe wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni na kwamba, wanatarajia kuufanyia kazi wakati wa mkutano wao wa kawaida, hapo Januari 2014. Baba Mtakatifu Francisko si kwamba, amechapisha ujumbe wa Mababa wa Sinodi juu ya Uinjilishaji Mpya kama njia ya kurithisha Imani ya Kikristo, bali ni mwaliko kwa Mama Kanisa kufanya toba na wongofu wa ndani, ili kuweza kukumbatia mabadiliko ya dhati, kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya, kwa kutambua kwamba, Kanisa kwa asili ni la Kimissionari.

Dr. Tveit anasema, Waraka huu unachangamotisha na ni mwaliko kwa Baraza la Makanisa Ulimwenguni ambalo hivi karibuni limehitimisha Mkutano wake mkuu uliokuwa ukifanyika mjini Busan, Korea ya Kusini, kuanza kuufanyia kazi. Ni Waraka unaoweka uwiano bayana kati ya tafakari kuhusu Kanisa, mitazamo ya Kimissionari na masuala ya uchumi, mazingira, haki na amani kama sehemu muhimu sana ya ujenzi wa Kanisa katika mtazamo wa Kimissionari.

Baraza la Makanisa Ulimwenguni katika mkutano wake wa kumi, lilibainisha umuhimu wa Kanisa kufanya toba na wongofu wa ndani; kwa kuwaendea wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na hali yao ya maisha na Kanisa kuanza kwa kasi na ari kubwa zaidi mchakato wa majadiliano ya kiekumene sanjari na kusimama kidete kulinda na kutetea misingi ya haki na amani. Hii ndiyo hija inayofanywa na Makanisa 345 wanachama wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni mara baada ya Maadhimisho ya Mkutano mkuu.

Kanisa Katoliki si mwanachama wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni anasema Dr. Tveit, lakini limeendelea kushirikiana kikamilifu na wajumbe wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni kwa njia ya Baraza la Kipapa la Uhamasishaji wa Umoja miongoni mwa Wakristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.