Kuna matumaini katika mapambano dhidi ya Ugonjwa wa Ukimwi, lakini bado kuna mengi
ya kufanywa!
Ugonjwa wa Ukimwi bado unaendelea kuwa ni tishio kwa familia nyingi Barani Afrika,
licha ya maendeleo makubwa yaliyokwisha kupatikana katika utoaji wa dawa za kurefusha
maisha. Waathirika wakubwa ni wanawake wanaolazimika kubeba mzigo wa huduma kwa familia
zao wakati wa shida na mahangaiko ya kuwatunza wagonjwa wa Ukimwi.
Bwana Ban
Ki- Moon, Katibu mkuu wa Umoja wa Matifa katika ujumbe wake wakati wa Maadhimisho
ya Siku ya Ukimwi Duniani kwa Mwaka 2013 anasema kwamba, Jumuiya ya Kimataifa ina
matumaini makubwa katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi na kwamba, kuna watu
millioni 14 ambao watapatiwa dara za kurefusha maisha hadi kufikia Mwaka 2015. Anasema,
bado kuna tatizo la unyanyapaa miongoni mwa watu na kwamba, kuna haja ya kuhakikisha
kuwa watu wengi zaidi wanapata dawa za kurefusha maisha.
Udhibiti wa maambukizi
ya virusi vya Ukimwi kutoka kwa Mama kwenda kwa mtoto ni jambo la muhimu sana, wakati
huu, Jumuiya ya Kimataifa inapojizatiti kupunguza maambukizi mapya ya Virusi vya Ukimwi.
Mkakati huu hauna budi kwenda sambamba na heshima kwa wanawake, kwa kukomesha vitendo
vyote vinavyowasababishia madhulumu na nyanyaso pamoja na kuwakinga dhidi ya maambukizi
ya Virusi vya Ukimwi.
Mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi, hayana budi kwenda
sanjari na vita dhidi ya ugonjwa wa Malaria na Kifua Kikuu; magonjwa yanayoendelea
kusababisha vifo vya watu wengi duniani, lakini zaidi miongoni mwa wananchi wanaotoka
katika nchi maskini zaidi duniani. Jumuiya ya Kimataifa inayo kazi kubwa mbele yake
ili kuhakikisha kwamba, Ukimwi unatokomezwa kutoka katika uso wa dunia!