2013-12-02 09:05:52

Maisha ya Kikristo ni hija ya upendo, udugu na mshikamano wa dhati kumwendea Kristo!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio, majira ya jioni alitembelea Parokia ya San Cirillo Alessandrino, iliyoko nje kidogo ya mji wa Roma. Parokiani hapo ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu Takatifu sanjari na kutoa Sakramenti ya Kipaimara kwa vijana tisa. Baba Mtakatifu amewakumbusha waamini kwamba, maisha yao ni hija ya kumwendea, ili hatimaye kukutana na Yesu Kristo, chemchemi ya furaha, amani na matumaini mapya, kwani Kristo aliyamimina maisha yake kwa ajili ya kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti.

Waamini wanakutana na Yesu katika maisha ya Sala, Sakramenti za Kanisa na matendo ya huruma. Amewakumbusha Wakristo walioimarishwa kwa Sakramenti ya Kipaimara kwamba, huo si mwisho wa kuuona mlango wa Kanisa kama wanavyofanya vijana wengi, lakini hii inapaswa kuwa ni mwendelezo wa hija ya kutaka kukutana na Yesu katika maisha ya kila siku kwa njia ya maisha adili na matendo mema. Baba Mtakatifu anasema, kwake ni furaha ya pekee kwani anaungana na waamini wengine kutembea ili kukutana na Yesu.

Maisha ya Kikristo ni hija ya upendo, udugu na mshikamano wa dhati ili kumwendea Kristo, anayepaswa kuwa ni kiongozi mkuu anayewaongoza waamini kwa upendo mkuu; anawajalia Sakramenti ya Upatanisho ili kuonja tena huruma na upendo wa Mungu, pale wanapojikuta wakitumbukia katika dhambi. Yesu ni tabibu wa kweli anayemponya mwanadamu kiroho na kimwili. Jambo la msingi kwa kila mwamini kutambua kuwa ni mdhambi, anayehitaji kuonjeshwa huruma na upendo wa Mungu kwa njia ya Kristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.