2013-12-02 10:27:29

Jubilee ya miaka 25 ya Jimbo kuu la Songea!


Jimbo kuu la Songea, Tanzania linaloundwa na Majimbo ya: Iringa, Lindi, Mbeya, Mbinga, Njombe na Tunduru- Masasi linasherehekea Jubilee ya Miaka 25 tangu lilipoanzishwa na Mwenyeheri Yohane Paulo II, kunako tarehe 18 Novemba 1987.

Kilele cha Maadhimisho haya hapo tarehe Mosi Desemba 2013, kimekwenda sanjari na Maadhimisho ya Kufunga Mwaka wa Imani, katika Ibada iliyoongozwa na Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Msimamizi wa Kitume wa Jimbo kuu la Songea ambaye pia ni Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania. Jimbo kuu la Songea lilibahatika kutembelewa na Mwenyeheri Yohane Paulo II, Septemba, 1990.

Katika mahubiri yake, Askofu Ngalalekumtwa amewataka waamini kujiandaa vyema ili kushiriki kikamilifu katika kipindi cha Majilio, kwa kufanya toba na wongofu wa ndani, tayari kumpokea Yesu Kristo Masiha anayekuja kuwatembelea katika maisha yao.

Askofu Ngalalekumtwa anasema, Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo inayojielekeza zaidi katika Uinjilishaji Mpya, waamini wanapewa nyenzo za kufanyia kazi kama sehemu ya mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu. Amewataka waamini kusoma, kutafakari na kulimwilisha Neno la Mungu kama njia ya kufika mbinguni.

Wamepewa Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki, muhtasari wa Imni, Sakramenti za Kanisa, Maisha adili na Maisha ya Sala, ni jukumu lao kuifahamu ili kutolea ushuhuda wa imani tendaji katika uhalisia wa maisha. Waamini wamekabidhiwa Nyaraka 16 za Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, wanazopaswa kuzifanyia kazi.







All the contents on this site are copyrighted ©.