2013-12-02 11:13:44

Changamoto zinazolikabili Kanisa Visiwani Antilles


Visiwa vya Caribbean ni kati ya maeneo ya Amerika ya Kusini yaliyobahatika kusikia Habari Njema ya Wokovu, yapata miaka 400 iliyopita. Visiwa hivi vinaundwa na watu kutoka katika lugha na tamaduni mbali mbali; watu ambao wana mielekeo tofauti ya kiuchumi na kijamii; historia na mwono wa maisha, mambo ambayo yasipoangaliwa kwa umakini mkubwa yanaweza kukwamisha mchakato wa Uinjilishaji Mpya Amerika ya Kusini.

Kanisa katika Visiwa hivi linakabiliwa na changamoto ya: upungufu mkubwa wa Mapadre na Watawa; kupungua kwa waamini wanaojitoa kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa pamoja na ukata unaokwamisha mikakati ya mipango ya maendeleo: kirohio na kimwili.

Hizi ni changamoto zinazopaswa kufanyiwa kazi, kwani Kanisa bila Mapadre, litachechemea katika shughuli mbali mbali za kichungaji: kiroho na kimwili. Maaskofu wanahaja ya kuwekeza zaidi katika kuhamasisha na kulea miito ya maisha ya Kipadre na Kitawa. Lengo hili linaweza kufanikiwa ikiwa kama vijana wa kizazi kipya wataonja furaha, ari na uaminifu wa Mapadre katika maisha na utume wao kwa Kristo na Kanisa lake.

Ni maneno ya Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu, alipokuwa anazungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki kutoka katika Visiwa vya Antilles, hivi karibuni wakati wa hija yake ya kichungaji nchini humo. Anasema, kuna uhaba wa Wakristo kutokana na ukweli kwamba, kuna makundi makubwa ya watu wanahama ili kutafuta fursa mpya za ajira; uhaba wa wahudumu wa Injili, na huduma hafifu zinazotolewa kwa waamini ni kati ya mambo yanayochangia baadhi ya waamini kukosa dira na mwelekeo katika maisha na utume wa Kanisa, matokeo yake ni waamini wengi kukimbilia katika Madhehebu ya Kikristo yanayoendelea kushamiri kwa kasi kubwa Amerika ya Kusini.

Kanisa Katoliki anasema Kardinali Filoni linaanza kupoteza utambulisho wake katika huduma za elimu na afya kwa kukosa wahudumu makini, jambo ambalo ni hatari kwa maisha na ustawi wa Kanisa. Maaskofu wanaalikwa kuwekeza zaidi katika majiundo ya waamini walei kwa njia ya vyama vya kitume, ili kuleta ari na mwamko mpya katika maisha ya Kanisa nchini humo.

Waamini bado wanahamasishwa kuchangia katika harakati za kulitegemeza Kanisa mahalia na kwamba, viongozi wa Kanisa waongozwe na ukweli na uwazi katika matumizi ya rasilimali na mali ya Kanisa. Maaskofu kamwe wasikate tamaa, bali wajifunge kibwebwe kutafuta tiba ya matatizo na changamoto hizi.

Maaskofu waguswe na mahitaji ya Mapadre wao na wawe tayari kuwaonesha upendo na huruma ya kibaba! Wajitahidi kuwapatia fursa za majiundo endelevu katika shughuli za kichungajik, maisha ya kiroho na kitamaduni.







All the contents on this site are copyrighted ©.