2013-11-30 08:58:14

Mikakati ya SECAM na CCEE kati ya Mwaka 2015 - 2017


Tume ya ushirikiano kati ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM pamoja na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Ulaya, CCEE, katika mkutano wao uliokuwa unafanyika mjini Roma, wameamua kufanya semina ya pamoja kati ya Maaskofu kutoka Barani Afrika na Ulaya, itakayofanyika mwezi Mei, 2015.

Itakuwa ni fursa kwa Maaskofu hawa kuweza kufanya tafakari ya kina kuhusu Waraka wa Kitume: Injili ya Furaha, Evangelii Gaudium uliotolewa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Francisko pamoja na changamoto zinazojitokeza katika maisha ya ndoa na familia, mambo yatakayojadiliwa kwa kina na mapana wakati wa Maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, itakayofanyika mjini Vatican, mwezi Oktoba 2014.

Washiriki katika semina hii watajikita zaidi katika changamoto ya kutangaza Furaha ya Familia. Maaskofu wataangalia tunu msingi za maisha ya ndoa na familia Barani Afrika na Ulaya. Hii inatokana na ukweli kwamba, Familia ni wadau wakuu wa mchakato wa Uinjilishaji Mpya. Familia pia zinapaswa kuinjilishwa ili ziweze kutekeleza wajibu na dhamana yake kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa. Maaskofu hawa pia watakuwa na semina kunako mwaka 2017.

Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki Cor Unum ameshiriki kwenye kikao cha kamati ya ushirikiano kati ya SECAM na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Ulaya.







All the contents on this site are copyrighted ©.