2013-11-30 11:21:26

Changamoto za kumtangaza Kristo katika nyakati za dijitali!


Baraza la Kipapa kwa ajili ya walei litaanza mkutano wake wa ishirini na sita wa mwaka hapo tarehe 5 hadi 7 Desemba 2013, kwa kuongozwa na kauli mbiu "Kumtangaza Kristo katika nyakati za Dijitali". Kwa mada hii, Baba Mtakatifu Francisko anapenda kuendeleza changamoto za Uinjilishaji katika ulimwengu wa mitandao, dhana iliyoanzishwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita.

Katika kipindi cha miaka kumi iliyopita, Kanisa limeendelea kutoa kipaumbele cha pekee katika njia za mawasiliano ya kijamii kama jukwaa linalopaswa kusaidia mchakato wa Uinjilishaji, lakini pia njia hizi zinapaswa kuinjilishwa. Wajumbme watapata fursa ya kupanga na kupitisha mikakati ya kichungaji itakayotekelezwa na Baraza hili kwa siku za usoni.

Baraza la Kipapa kwa ajili ya walei linasema, kwamba, waamini walei ni wadau wakuu katika matumizi ya njia za mawasiliano ya kijamii. Wanahamasishwa na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, wanachangia kikamilifu katika Kuinjilisha mitandao ya kijamii kadiri ya mpango wa Mungu na kama sehemu ya binadamu kuweza kukutana na Yesu Mkombozi wa dunia. Waamini walei wanapaswa kutambua changamoto kubwa iliyoko mbele yao kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari.

Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa Kitume, Injili ya Furaha, Evangelii Gaudium anawataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kutambua dhamana na wajibu wa Kanisa kwamba, ni la Kimissionari na linatumwa kwenda kutangaza Kweli za Kiinjili hadi miisho ya dunia. Njia ya mawasiliano ni nyenzo muhimu sana katika utekelezaji wa dhamana na utume wa Kanisa na kwamba, watu wanahitaji kusikia na kuonja ile Injili ya Furaha.

Wawezeshaji waliochaguliwa kushiriki katika mkutano wa ishirini na sita ni watu wenye weledi, uzoefu na mang'amuzi makubwa katika masuala ya mitandao ya kijamii. Wajumbe wataangalia fursa, changamoto na matatizo yanayojitokeza kutokana na matumizi ya mitandao ya kijamii hasa miongoni mwa vijana wa kizazi kipya. Licha ya magumu yote haya, lakini Kanisa halina budi kuwa mstari wa mbele katika matumizi ya mitandao ya kijamii kama jukwaa la kutangaza INJILI YA FURAHA.

Baadhi ya mada zitakazojadiliwa ni pamoja na: Utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu katika Ulimwengu wa utandawazi; dunia ya mitandao, muundo wa kisaikolojia na utambulisho wa watu. Kwa hakika, wajumbe wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya walei linataka kuzama zaidi katika matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii kama jukwaa la Uinjilishaji Mpya.







All the contents on this site are copyrighted ©.