2013-11-29 11:58:20

Madhulumu ya waamini wa dini ya Kiislam nchini Angola?


Serikali ya Angola imekanusha tetesi kwamba, ilikuwa na mpango wa kufunga misikiti yote nchini Angola kwa kukosa usajili si za kweli na kwamba, Serikali haina mpango wa kuwadhulumu wala kuwanyanyasa waamini wa dini ya Kiislam nchini Angola. Ufafanuzi huu umetolewa na Bwana Manuel Fernando, Mkurugenzi wa taasisi ya kitaifa ya masuala ya kidini, Wizara ya Utamaduni nchini Angola.

Tetesi kwamba, Serikali ya Angola inataka kufunga misikiti yote nchini humo kwa vile haikusajiliwa zimepokelewa kwa hisia tofauti na watetezi wa haki msingi za binadamu, kwani ikiwa kama uamuzi huu utatekelezwa unaweza kusababisha mtafaruku mkubwa miongoni mwa wananchi wa Angola. Serikali pia inasemekana kuwa na mpango wa kufuta madhehebu ya Kikristo yasiyosajiliwa na yale ambayo yanakwenda kinyume cha mila, desturi na tamaduni njema za Angola.

Bi Rosa Cruz e Silva, Waziri wa habari nchini Angola amenukuliwa na vyombo vya habari akisema kwamba, Dini ya Kiislam haikupata usajili nchini Angola kadiri ya sheria za nchi. habari hizi zimechafua hali ya hewa kwa Serikali kushutumiwa kwamba, inaendesha madhulumu ya kidini dhidi ya waamini wa dini ya Kiislam. Sheria inaonesha kwamba, ili kikundi cha waamini wa dini yoyote nchini Angola kiweze kuendesha shughuli zake lazima kwanza kabisa kisajiliwe Serikalini. Ikiwa kama sheria hii itatekelezwa zaidi ya misikiti 70 itabomolewa!

Takwimu zinaonesha kwamba, Angola ina wananchi wapatao millioni 19. kati yao kuna: wakristo millioni 17. 2; Waislam 40, 000; 10, 000 Wabudha na Waebrania. Baadhi ya waamini wanashindwa kupata kibali cha Serikali kutokana na kushindwa kukidhi masharti ya sheria za nchi. Wachunguzi wa mambo wanasema sheria hii haitekelezeki.







All the contents on this site are copyrighted ©.