2013-11-28 11:36:40

Baba Mtakatifu Francisko anapania kuwaimarisha wanafunzi katika azma ya Uinjilishaji Mpya


Zaidi ya wanafunzi 10,000 kutoka katika Vyuo Vikuu na Taasisi za elimu ya juu zilizoko mjini Roma wanatarajiwa kushiriki katika Ibada ya Masifu ya kwanza ya Kipindi cha Majilio, yatakayoongozwa na Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi, majira ya jioni kuanzia saa 11:30 kwa saa za Ulaya. Haya ni Mapokeo kwa Baba Mtakatifu kukutana na wanafunzi kabla ya Noeli, ili kuwaandaa vyema zaidi katika kipindi cha Majilio.

Kama sehemu ya maandalizi haya, Kardinali Agostino Vallini, Makamu Askofu Jimbo kuu la Roma atapokea Sanamu ya Bikira Maria Kikao cha Hekima na kuongoza tafakari ya Rozari takatifu, muhtasari wa Injili.

Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Sanamu ya Bikira Maria Kikao cha Hekima, ilitunzwa na wanafunzi kutoka Brazil kama sehemu ya ushiriki wao kwa Maadhimisho ya Siku ya Vijana iliyofanyika Mwezi Julai, 2013, mjini Rio de Janeiro, Brazil. Mwaka huu, Wanafunzi kutoka Ufaransa ndio watakaokaabidhiwa Sanamu hii tayari kuitembeleza kwenye vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu nchini Ufaransa.

Wakati huo huo, Askofu Lorenzo Leuzzi anatarajia siku ya Ijumaa usiku kuongoza Ibada ya Misa takatifu kwenye Chuo Kikuu cha Tor Vergata. Ibada ya Masifu ya Jioni itakaoongozwa na Baba Mtakatifu Francisko ni tukio muhimu sana kwa wanafunzi wa vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu, kwani Baba Mtakatifu anapenda kuitumia fursa hii kuwahimiza wanafunzi kuwa wadau wakuu wa Uinjilishaji miongoni mwa wanafunzi wenzao katika Vyuo Vikuu na Taasisi za Elimu ya Juu







All the contents on this site are copyrighted ©.