2013-11-26 07:57:01

Watu wanaonesha imani, ukarimu na mshikamano wa dhati licha ya majanga yanayowakabili


Licha ya taabu na magumu ambayo wananchi wa Ufilippini wanakabiliana nayo kwa sasa, lakini bado ni watu wenye imani, ukarimu na mshikakano wa dhati kati yao. Hayo yamesemwa na Monsinyo Paul Tighe, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii ambaye kwa sasa yuko nchini Ufilippini kuhudhuria Kongamano la pili la Vyombo vya mawasiliano ya Jamii nchini Ufilippini.

Monsinyo Tighe anasema kwamba, vyombo vya habari vimekuwa mstari wa mbele kuhabarisha yale yaliyokuwa yanajiri nchini Ufilippini baada ya kukumbwa na tufani kali, iliyosababisha maafa makubwa kwa maisha ya watu pamoja na miundo mbinu kiasi kwamba, watu wengi bado wanahitaji msaada wa dharura ili kukabiliana na majanga haya! Mawasiliano haya yamewagusa wengi na watu wakajitoa kuonesha mshikamano wao a dhati, kama walivyofanya waamini wakati wa kufunga Mwaka wa Imani kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican tarehe 24 Novemba 2013.

Vatican kwa njia ya mashirika yake ya misaada kitaifa na kimataifa inaendelea kuwahamasisha waamini na watu wenye mapenzi mema kuchangia kwa hali na mali katika harakati za kuwasaidia waathirika wa tufani nchini Ufilippini. Huu ndio mwelekeo wa ujumla kwa waamini kutoka Majimbo na Parokia mbali mbali duniani. Mwaka wa Imani imekuwa ni fursa ya kujenga na kuimarisha mshikamano wa upendo kati ya watu!

Monsinyo Tighe anasema, kuna haja kwa Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, anatumia kikamilifu maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari kwa ajili ya kutangaza kweli za Kiinjili. Ili kufanikisha azma hii kuna haja ya kufahamu lugha ya wale watu wanaoishi kwenye ulimwengu wa mitandao. Mambo makuu matatu ya kuzingatiwa ni: kuzungumza, kushirikishana na kujadiliana. Watu wanaoishi katika ulimwengu wa mitandao wasaidiwe kujenga utamaduni wa majadiliano na kujitahidi kuishi kadiri ya tunu msingi za Kiinjili.








All the contents on this site are copyrighted ©.