2013-11-26 08:21:50

Rais Putin akutana na kuzungumza na Papa Francisko mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu jioni tarehe 25 Novemba 2013 amekutana na kuzungumza na Rais Vladimir Putin wa Russia. Baadaye Rais Putin na ujumbe wake walikutana na kuzungumza na Askofu mkuu Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyeambatana na Askofu mkuu Dominique Mamberti, katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.

Katika mazungumzo yao, viongozi hawa wawili wameelezea kuridhishwa kwao na uhusiano uliopo baina ya nchi hizi mbili na baadaye, walijadili mambo yanayogusa mafao ya pande hizi mbili, hususan maisha ya Waamini wa Kanisa Katoliki nchini Russia na mchango wa Wakristo katika ustawi na maendeleo ya Russia. Wamejadili pia hali ngumu inayowakabili Wakristo sehemu mbali mbali za dunia; umuhimu na kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu; uhai sanjari na tunu msingi za maisha ya kifamilia.

Viongozi hawa kwa namna ya pekee kabisa wamejadili kuhusu mchakato wa amani Mashariki ya Kati na hali tete nchini Syria. Rais Putin amemshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa barua kwa wakuu wa G20 wakati wa mkutano wao uliofanyika mjini Pitsburg. Wamekubaliana kimsingi kusitisha vita, kuendelea kutoa huduma na misaada ya kiutu kwa waathirika pamoja na kukazia majadiliano yanayolenga upatikanaji wa suluhu ya kudumu nchini Syria. Majadiliano haya yawahusishe wadau mbali mbali ili amani ya kweli iweze kupatikana.







All the contents on this site are copyrighted ©.