2013-11-26 09:46:33

Msivumishe habari zisizo na msingi katika hali tete kama Nigeria!


Kardinali John Onaiyekan, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria anasema, hana uhakika na uvumi uliosambazwa na baadhi ya vyombo vya habari ndani na nje ya Nigeria kuhusu wanawake wa Kikristo kutekwa nyara na kulazimishwa kuolewa na wanajeshi wa Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram. Anakiri kwamba, wanawake kutekwa na kubakwa ni vitendo vinavyoendelea nchini Nigeria, hali inayodhalilisha utu na heshima ya wanawake.

Kardinali Onaiyekan anasema hajui kama kuna kampeni ya kuwakamata wanawake wa Kikristo na kuwalazimisha kuolewa na wanajeshi wa Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram. Inasikitisha kusikia watu wakisambaza habari za uvumi na uchochezi katika mazingira kama ya Nigeria ambako hali ni tete kutokana na madhulumu ya kidini dhidi ya Wakristo. Anawataka waandishi wa habari kusema ukweli badala ya kutunga habari zinazoweza kusababisha mtafaruku ndani ya Jamii.

Kardinali Onaiyekan anasema, hivi karibuni, Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram kimepata pigo kubwa kutoka kwa Jeshi la Serikali, katika Mikoa ya Kaskazini mwa Nigeria. Kikundi hiki kinaanza kupoteza mwelekeo na dira yake, si kama ilivyokuwa miezi kadhaa iliyopita.

Lakini anasema Kardinali John Olorunfemi Onaiyekan, hii haimaanishi kwamba, Boko Haram imesambaratishwa, bali bado kuna vitendo vya ujambazi vinavyofanywa na makundi ya Askari na wala si Jeshi la Msituni kama Boko Haram ilivyokuwa mwanzoni.







All the contents on this site are copyrighted ©.