2013-11-26 08:33:17

Bi Mary Robinson akutana na Rais Jakaya Kikwete


Rais Jakaya Mrisho Kikwete Jumatatu tarehe 25 Novemba 2013 amefanya mazungumzo na Bibi Mary Robinson, Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) katika eneo la Maziwa Makuu. Mazungumzo baina ya Rais Kikwete na Bibi Robinson yamehusu maendeleo na hatua iliyofikiwa katika mgogoro wa Mashariki mwa DRC - Congo na jitihada zinazofanywa za kutekeleza mkataba wa amani ambapo Tanzania imetoa mchango mkubwa katika jitihada hizo.
"Nakupongeza kwa juhudi zako katika masuala ya amani katika nchi za Maziwa Makuu na pia nakuomba uendelee kutoa mchango wako zaidi wa mambo gani muhimu ya kuzingatia baadaye”. Bibi Robinson pia amempa salamu za rambirambi Rais Kikwete pamoja na familia za wanajeshi waliopoteza maisha yao katika harakati za kuleta amani huko mashariki mwa DRC Congo.

Bibi Robinson amemwomba Rais Kikwete aendelee kutoa mchango wake kwenye juhudi za kuleta amani nchini Congo baada ya kikosi cha UN kufanikiwa kuwaondoa waasi wa kikundi cha M23 kutoka Mashariki mwa DRC – Congo. Viongozi hawa wamekubaliana kuwa ipo haja ya kuendeleza juhudi za kuleta amani DRC na kuangalia jinsi ya kusonga mbele na kubainisha mahitaji na hatua zaidi za kuchukua katika kuhakikisha amani na usalama vinapatikana na hatimaye kujenga uchumi wa DRC.

Wakati huo huo Rais Kikwete amekutana na Rais Mstaafu wa Msumbiji Mheshimiwa Joachim Chissano ambaye ni msuluhishi wa mgogoro wa Mpaka Kati ya Tanzania na Malawi katika Ziwa Nyasa. Rais Chissano na ujumbe wake upo nchini kusikiliza hoja za Tanzania kuhusu mpaka wa Ziwa Nyasa ambapo Rais Kikwete amewasilisha hoja zake kwao. Tayari msuluhishi huyo ameshasikiliza hoja za Malawi ambapo inatarajiwa hoja za nchi zote mbili hizi zitatafsiriwa na kuzingatiwa katika kutafuta suluhu ya mgogoro huo wa Ziwa Nyasa.








All the contents on this site are copyrighted ©.