Kanisa la Anglikani Tanzania limepata pigo la kufiwa na Askofu John Simalenga (60)
wa Dayosisi South West Tanganyika iliyopo Njombe, Mkoani Iringa. Akizungumza na waandishi
wa habari mjini Dodoma Katibu mkuu wa Kanisa Anglikani Tanzania Canoni Dk. Dickson
Chilongani alisema kuwa Kanisa limepata pigo kubwa kutokana na kifo cha Askofu Simalenga
ambaye aliugua kwa muda mfupi.
Alieleza kuwa kifo cha Askofu Simalenga kimetokea
Novemba, 24, 20013 muda mfupi baada ya kuruhusiwa kutoakatika hospitaliya ya kanisa
hilo iliyopo Njombe. Alisema kuwa askofu alianza kuumwa alikwenda hospitali kwa ajili
ya kupima afya yake na alipofika hospitali ilibainika kuwa alikuwa na maralia pamoja
na sukari kupanda hadi kufikia 30 huku shinikizo la moyo kuwa juu.
Canon Dk.
Chilongani alisema kuwa baada ya madaktari kubaini kwamba Askofu anasumbuliwa na matatizo
hayo alipewa dawa na kuruhusiwa kwenda nyumbani wakitegemea kuwa dawa hizo zingemsaidia
kutuliza magonjwa ambayo alibainika kuwa nayo. Alisema kinyume na matarajio ya madaktari,
Askofu Simalenga baada ya kurudi nyumbani hali ilibadilika ghafla na kufariki dunia
majira ya saa 11 alfajiri.
Marehemu Askofu John Simalenga alizaliwa tarehe
30 Novemba 1953 na kufariki dunia tarehe 24 Novemba 2013. Alisema Kanisa Anglikani
linaendelea na taratibu za maandali ya utaratibu wa mazishi ya mwili wa askofu huyo
ikiwa ni pamoja na kuendelea kutoa taarifa kwa wachungaji pamoja na viongozi mbalimbali
wa dini na Serikali.