Halmashauri walei Jimbo kuu la Dar es Salaam wala kiapo!
Katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Kristo Mfalme sanjari na kilele cha Mwaka wa Imani,
Askofu msaidizi Titus Mdoe wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, aliendesha Ibada ya Misa
Takatifu kwa ajili ya kuwasimika viongozi wa Halmashauri Walei Jimbo kuu la Dar es
Salaam. Ibada hii imefanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Yosefu, Dar es Salaam.
Katika mahubiri yake, Askofu msaidizi Mdoe aliwakumbusha viongozi wa Halmashauri
ya Walei dhamana na wajibu wao katika maisha na utume wa Kanisa; akawataka kuwa mstari
wa mbele katika kuonesha dira na mwanga utakaosaidia mchakato wa utekelezaji wa maamuzi
mbali mbali yanayofanywa kwa ajili ya maendeleo na ustawi wa Familia ya Mungu Jimbo
kuu la Dar es Salaam.
Askofu msaidizi Mdoe anasema, Yesu Kristo ni Mfalme wa
Ukweli na uzima; Utakatifu na neema; haki, mapendo na amani. Kama viongozi wa Kanisa
wametwaliwa kati ya watu kwa ajili ya kusimamia maisha na utume wa Kanisa, changamoto
ya kumpenda Mungu na watu wake. Familia ya Mungu Jimbo kuu la Dar es Salaam imewaamini
na kuwathamini kwa kuwakabidhi majukumu haya mazito baada ya Maadhimisho ya Mwaka
wa Imani, mwaliko kwao wa kuwatumikia kwa moyo wa uchaji, unyenyekevu na pasi na makuu.
Amewataka
viongozi wa Halmashauri Walei Jimbo kuu la Dar es Salaam kumwiga Kristo aliyejinyenyekesha
hata akajitwalia hali ya ubinadamu, katika mambo yote akawa sawa na binadamu, lakini
hakutenda dhambi; alitii hata kukubali kifo cha Msalaba, kielelezo cha kiongozi makini
aliyewapenda watu wake upeo! Alionesha mfano wa uongozi kwa njia ya mifano ya maisha
yake, hata wao wanapaswa kuwa kweli ni watumishi wa Familia ya Mungu, Jimbo kuu la
Dar es Salaam.
Kamwe wasitake kuwa ni Mabwana na wakandamizaji, kwani uongozi
ni safari ya maisha! Wasiwe ni viongozi wa kwanza "kutupa madongo" kwa Maparoko wao,
bali kwa unyenyekevu na moyo mkuu wajitafiti kwanza mioyoni mwao ikiwa kweli wametekeleza
wajibu wao kama waamini walei na viongozi wa Kanisa.
Askofu msaidizi Titus
Mdoe amewataka viongozi Halmashauri Walei Jimbo kuu la Dar es Salaam kuhakikisha kwamba,
wanasoma na kutafakari Neno la Mungu, tayari kulimwisha katika uhalisia wa maisha
yao, pili wanaifahamu vyema Katekisimu ya Kanisa Katoliki, dira na mwongozo wa maisha
yao ya kiroho; tatu, wajitahidi kuyafahamu Mafundisho Jamii ya Kanisa, tayari kushiriki
katika mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu. Kimsingi Askofu msaidizi Titus Mdoe
anasema, ni nyenzo zinazoweza kuwasaidia kutekeleza wajibu wao kama viongozi wa Halmashauri
Walei Jimbo kuu la Dar es Salaam.