2013-11-25 07:29:25

CUEA wahitimisha Mwaka wa Imani


Askofu mkuu Charles Daniel Balvo, Balozi wa Vatican nchini Kenya, hivi karibuni amehitimisha Mwaka wa Imani kwa Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki Afrika Mashariki na Kati, CUEA kwa Ibada ya Misa Takatifu pamoja na kuwapokea Wakatekumeni wapya kumi na watu ambao wameanza hija ya maisha ya kiroho, wakitaka kuingia kwenye Mlango wa Imani, ili hatimaye, wapokee Sakramenti ya Ubatizo. Wakatekumeni hawa ni kutoka katika Jumuiya ya Chuo Kikuu cha CUEA.
Askofu mkuu Balvo amewakabidhi Wakatekumeni wapya Biblia Takatifu, ili Neno la Mungu liweze kuwaangazia katika mapito ya maisha yao, kwa kujitahidi kumfahamu Kristo kwa njia ya Maandiko Matakatifu, ili siku moja waweze kumtolea ushuhuda wa kweli.
Wakatekumeni hao wamepewa Msalaba, kielelezo cha Fumbo la Ukombozi, mahali ambapo hekima ya Mungu imetundikwa juu yake. Wanaalikwa kumwangalia Kristo aliyeyamimina maisha yake kwa ajili ya kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti na hivyo kuwajalia tena uwezo wa kufanyika watoto wateule wa Mungu.
Askofu mkuu Balvo katika mahubiri yake ameendelea kukazia kwamba, imani ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu na ni sehemu ya maisha ya mwanadamu na Kanisa. Imani hii inaweza kurutubishwa kwa njia ya Neno la Mungu, Sakramenti, Maisha adili yanayoongozwa na Amri za Mungu pamoja na Sala inayojidhihirisha katika matendo.
Wakatekumeni na Wakristo katika ujumla wao, waendelee kuimarika katika imani, wakati wa raha na karaha; wakati wa afya na magonja, daima Mwenyezi Mungu apewe kipaumbele cha kwanza. Jumuiya ya Wakristo wanaoishi CUEA wameombwa kuwasaidia Wakatekumeni wapya katika hija ya maisha yao, ili hatimaye, waweze kupata ukomavu.
Naye Monsinyo Pius Rutechura, Makamu mkuu wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki Afrika Mashariki na Kati, CUEA, amemshukuru Askofu mkuu Balvo kwa kuwapatia heshima ya kutembelea CUEA na kushiriki katika Ibada ya Misa Takatifu kama kielelezo cha kufunga Mwaka wa Imani, tayari kuendeleza neema na baraka ambazo waamini wamejipatia wakati wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani.








All the contents on this site are copyrighted ©.