Ugonjwa ni mahali pa kuonja fadhila za Kimungu: imani, matumaini na mapendo!
Askofu mkuu Zygmunt Zimowski katika tafakari yake wakati wa Maadhimisho ya Mkutano
wa XXVIII wa Kimataifa uliondaliwa na Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa
wafanyakazi katika sekta ya afya uliohitimishwa mwishoni mwa Juma, anasema, Maadhimisho
ya Mwaka wa Imani ni chachu ya kuendeleza mambo msingi ambayo waamini wametafakari
na kuonja katika hija ya maisha yao ya kiroho na kimwili kwa mwaka mzima, ili waweze
kuyaendeleza kwa siku za usoni kadiri ya Mpango wa Mungu.
Anawahamasisha wagonjwa
na wale waliokata tamaa ya maisha kutokana na shida na majaribu mbali mbali, kuutafuta
tena mwanga wa imani unaojikita katika upendo na matumaini ya kweli kwa Mwenyezi Mungu,
daima wakiwa tayari kupokea na magonjwa kama sehemu ya kushiriki katika kazi ya ukombozi,
iliyoanzishwa na Kristo mwenyewe kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko wake! Imani anasema
Baba Mtakatifu Francisko, iwe ni dira na mwanga wa maisha ya waamini kwa kutambua
kwamba, kwa hakika Mwenyezi Mungu anawapenda na kuwathamini hata katika magonjwa na
mahangaiko yao ya ndani!
Ugonjwa unaweza kuwa ni mahali muafaka pa kuonja na
kufanya mang'amuzi ya kweli za kiimani pamoja na mahusiano ya kibinadamu ndani ya
Jamii. Kuna umuhimu wa kuonesha ubinadamu unaojali na kuguswa na mahangaiko ya wengine
na kwa namna ya pekee kabisa wagonjwa na wale wasiokuwa na msaada. jambo la kusikitisha
ni kuona ukatili unaoendelea kufanywa dhidi ya wagonjwa kana kwamba, wao wamependa
kuwa katika hali hii na wengi wanasahau kwamba, kabla hujafa, bado mwanadamu hujaumbika!
Askofu
mkuu Zygmunt anaendelea kubainisha kwamba, ugonjwa ni mahali pa kuonja kwa namna ya
pekee zile fadhila za Kimungu, yaani: imani, matumaini na mapendo. Katika mateso na
mahangaiko ya ndani, mgonjwa anaweza kuwa ni kielelezo makini cha imani kwa Kristo
na Kanisa lake, lakini pale anapokata tamaa matokeo yake ni kukimbilia kwa wachawi
na imani za kishirikina.
Waamini watambue na kuonja nguvu na ukuu wa Mungu
hata katika mateso na magonjwa yao, kwani Yeye ana uwezo wa kuwainua na kuwanyanyua
tena. Magonjwa ni sehemu ya maisha ya mwanadamu, lakini yanaweza kupatiwa maana kadiri
ya imani na matumaini aliyo nayo mgonjwa mwenyewe. Imani inamwangazia mgonjwa hata
katika giza la undani wa maisha yake, kwa kutambua kwamba, daima Mwenyezi Mungu anafanya
hija na watu wake, kamwe hawezi kuwatelekeza, jambo la msingi ni kufungua macho ya
imani, ili kutambua uwepo wa Mungu anayeokoa na kuponya.
Wagonjwa wapate faraja
kutoka katika familia na Jamii inayowazunguka anasema Askofu mkuu Zygmunt Zimowski
katika tafakari yake kwa wajumbe waliokuwa wanahudhuria mkutano wa kimataifa wa XXVIII
uliokuwa unajadili pamoja na mambo mengine mchango wa Kanisa katika kuwahudumia wazee
wagonjwa!