2013-11-24 08:47:02

Mwaka wa Imani: Imani na Kifodini!


Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, waamini wamepata fursa ya kusikiliza shuhuda na changamoto katika hija ya imani mintarafu historia ya Kanisa. Waamini wengi hasa kutoka Makanisa ya Mashariki walishuhudia imani yao kwa Kristo kwa njia ya kumwaga damu.

Hii ni kutokana ukweli kwamba, Mwanga ambao ni Kristo ulikuja kuleta nuru ulimwenguni, lakini kwa bahati mbaya mwanadamu akapenda kugandamana na giza na kuitema zawadi ya mwanga. Yesu ambaye ni Mkombozi na chemchemi ya matumaini ya ulimwengu akawekwa pembeni utadhani ni gari bovu!

Ni sehemu ya hotuba iliyotolewa na Kardinali Leonardi Sandri, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki wakati alipokuwa anashiriki kwenye Kongamano lililoandaliwa na Kanisa Katoliki la Kigiriki kutoka Romania kwa kuongozwa na kauli mbiu "Imani na Kifodini" wakati wa utawala wa Kikomunisti nchini Romani. Mama Kanisa anamshukuru Mwenyezi Mungu kwa ajili ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani ambayo yametoa nafasi kwa waamini kufanya tafakari ya kina, kutolea ushuhuda wa imani tendaji pamoja na kusonga mbele, huku wakitembea katika mwanga wa Kristo Mfufuka.

Kardinali Sandri anasema, viongozi wa Kanisa waliwaandaa watu kusimama kidete kulinda na kutetea imani yao hata ikiwabidi kutolea sadaka ya maisha! Maandalizi haya yalijikita katika mahubiri kwenye Ibada za Misa takatifu, hija za kichungaji zilizofanywa na Maaskofu Maparokiani, hija za maisha ya kiroho pamoja na barua za kichungaji zilizowahamasisha waamini kutoa kipambele cha kwanza kwa Kristo na Kanisa lake, matokeo ni watu wakaimarika katika imani kiasi cha kujitosa kimasomaso kukabiliana na udhalimu wa nyakati zile.

Kilele cha madhulumu haya ni mwaka 1948 Wakristo walipohukumiwa kwa "mpigo" kifo dini bila hata ya kesi yao kusikilizwa. Waamini waliteseka na kumwaga damu yao kwa ajili ya Kristo, Kanisa na Khalifa wa Mtakatifu Petro. Kila Askofu akawa imara na wala hakukubali kumsaliti Kristo na Kanisa lake, changamoto ya kuendelea kudumisha misingi thabiti ya imani, kiasi hata cha kutolea ushuhuda katika imani tendaji bila kusahau kukuza majadiliano ya kidini na kiekumene, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.







All the contents on this site are copyrighted ©.