2013-11-24 09:39:34

Kampeni ya amani katika Eneo la Maziwa Makuu kuzinduliwa hapo tarehe Mosi, Desemba 2013


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika ya Kati, ACEAC, linalounganisha nchi za: DRC, Burundi na Rwanda, linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kushuhudia imani yao kwa Yesu Kristo na Kanisa lake; kuanzisha mchakato wa ujenzi wa mshikamano na mfungamano wa kijamii pamoja na kusaidia majiundo makini ya dhamiri nyofu, ili watu waweze kusamehe na kusahau sanjari na kujenga utamaduni na misingi ya haki, amani na upatanisho wa kitaifa!

Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu katoliki Afrika ya Kati, hapo tarehe Mosi Desemba 2013, Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio, litazindua mpango mkakati unaopania kujenga na kudumisha misingi ya amani kwenye Eneo la Maziwa Makuu, tukio hili litafanyika mjini Goma, Kaskazini mwa Kivu. Takwimu zinaonesha kwamba, nchini DRC kuna jumla ya watu millioni 5 waliofariki dunia katika kipindi cha miaka kumi na mitano iliyopita na watu zaidi ya millioni mbili na nusu hawana makazi ya kudumu. Idadi ya nyanyaso na madhulumu dhidi ya wanawake katika eneo hili inazidi kuongezeka kutokana na vita pamoja na machafuko ya kisiasa na kijamii.

Vyama vya kiraia hivi karibuni, viliiomba Serikali ya DRC Jumuiya ya Kimataifa na Majeshi ya waasi kuhakikisha kwamba, wanapata suluhu ya kudumu, ili amani iweze kutawala tena nchini DRC kwani kinzani, migogoro na vita ni "janja" ya watu wacheche wanaoendelea kufaidi wakati mamillioni ya watu yanateseka kutokana na vita. Mkakati wa amani kwenye Eneo la Maziwa Makuu unaungwa mkono pia na viongozi wa Kanisa Anglikani na uko wazi kwa watu wenye mapenzi mema kuchangia ili amani ya kweli iweze kupatikana.

Ufafanuzi huu umetolewa na Askofu Fridolin Ambongo Besungu wa Jimbo la Bokungu - Ikela, Mwenyekiti wa Tume ya Haki na Amani, Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika ya kati na Mratibu wa Kampeni "Amani katika Eneo la Maziwa Makuu". Viongozi wa kidini nchini DRC wanawapongeza wadau mbali mbali kutokana na mafanikio yaliyopatikana hivi karibuni baada ya ngome ya M23 kuchakazwa vibaya.

Jumuiya ya Kimataifa haina budi kuunga mkono juhudi za kutafuta amani ya kudumu nchini DRC sanjari na kuanza mchakato wa: haki, amani, upendo na upatanisho wa kweli. Watu wajifunze kuheshimu haki msingi za binadamu sanjari na kujenga utamaduni wa amani na utekelezaji wa dhamana kwa kila mtu ndani ya Jamii.

Viongozi wa kidini wanataka kurusha karata yao katika mchakato wa kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na upatanisho wa kitaifa nchini DRC, kwa kuwahusisha waamini wa Makanisa yao, viongozi wa kisiasa na kiserikali pamoja na watu wote wenye mapenzi mema. Jitihada hizi ni ushirikiano na Mashirika ya misaada ya kiutu CAFOD kutoka Uingereza na CatholicRelief Service, CRC kutoka Marekani.







All the contents on this site are copyrighted ©.