Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wahudumu wa sekta ya afya
katika Maadhimisho ya Mkutano wa XXVIII wa Kimataifa, uliokuwa unafanyika mjini Vatican
kuanzia tarehe 21 hadi tarehe 23 Novemba 2013, limezindua kitabu cha msaada kwa ajili
ya wahudumu wa sekta ya afya na Uinjilishaji Mpya kama njia ya kutangaza imani.
Msaada
huu wa kichungaji unaongozwa na kauli mbiu "Nendeni, mkafundishe na kuwaponya wagonjwa,
Injili kama ilivyoandikwa na Mathayo. 10: 6-8. Kauli mbiu hii kwa lugha ya Kilatini
inasomeka kama ifuatavyo: "Euntes docete et curate infirmos". Huu ndio msingi wa utume
wa Mama Kanisa katika kuwahudumia wagonjwa kama alivyofundisha Yesu mwenyewe kwa wafuasi
wake.
Wagonjwa wanapaswa kushibishwa kwa utamu wa Neno la Mungu na tiba muafaka
ndivyo anavyofafanua Askofu mkuu Zygmunt Zimowski, Rais wa Baraza la Kipapa la shughuli
za kichungaji kwa ajili ya wahudumu wa sekta ya afya wakati wa kuzindua kitabu hiki
kinachopania kuwa ni msaada wa kichungaji kwa ajili ya huduma kwa wagonjwa, wakati
huu Mama Kanisa anapojielekeza zaidi katika azma ya Uinjilishaji Mpya.
Huduma
ya Neno la Mungu na tiba ni mambo yanayokwenda pamoja, lakini kwa namna ya pekee wakati
huu wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani sanjari na mwendelezo wa mchakato wa Uinjilishaji
Mpya, changamoto kubwa kwa Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.
Vituo vya huduma ya afya vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Mama Kanisa ni mahali
muafaka pa Uinjilishaji; mahali ambapo watu wanaweza kuonja upendo na huruma ya Mungu
kwa njia ya jirani zao. Wahudumu wa sekta ya afya watambue kwamba, wao ni watume wa
huruma ya Mungu kati ya watu wanaoteseka na kusumbuka!
Monsinyo Jean Marie
Mupendawatu, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya
wahudumu wa sekta ya afya anasema, mikakati ya kichungaji katika sekta ya afya na
Uinjilishaji kama sehemu ya mchakato wa kutangaza imani ni mambo muhimu sana kwa Mama
Kanisa kwa wakati huu. Hiki ni kitabu chenye kurasa 48 ambazo zimesheheni tafakari
za kina mintarafu Mwaka wa Imani na Uinjilishaji Mpya.
Huu ni msaada wa pekee
kabisa kwa wahudumu wa sekta ya afya, watu wa kujitolea pamoja na familia zenye wagonjwa,
zinazo tamani kufanya maboresho ya huduma ya kiroho wanayotoa kwa ajili ya wagonjwa
wanaowahudumia. Kitabu hiki kimezinduliwa wakati wa mkutano wa Kimataifa wa XXVIII
uliokuwa unaongozwa na kauli mbiu "Kanisa kwa ajili ya huduma kwa wazee wagonjwa:
tiba kwa wagonjwa walioathirika na magonjwa ya mishipa ya fahamu. Kitabu hiki ni mwendelezo
wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, ambao unafungwa rasmi kwa Siku kuu ya Yesu Kristo
Mfalme wa Ulimwengu.
Kitabu kinajikita zaidi katika mikakati ya shughuli za
kichungaji kama sehemu muafaka ya Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima:
kiroho na kimwili, anasema Monsinyo Mupendawatu. Mama Kanisa anapenda kushika hatamu
katika kukabiliana na changamoto zinazoibuliwa kwenye ulimwengu wa utandawazi na maendeleo
ya sayansi na teknolojia; ili kuyatakatifuza malimwengu!
Umefika wakati wa
kuanza tena maisha mapya kwa Yesu Kristo kwa njia ya kusoma, kuitafakari na kuimwilisha
Injili ya Huruma ya Mungu katika kila hatua ya historia ya maisha ya mwanadamu na
kwamba, matunda yake ni: toba na wongofu wa ndani, faraja na matumaini yasiyodanganya
kamwe!