2013-11-23 08:12:09

Imani na amani ni chanda na pete, kamwe haviwezi kutenganishwa!


Askofu mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha, Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican wakati huu Mama Kanisa anapofunga Mwaka wa Imani anabainisha kwamba, Siku kuu ya Yesu Kristo Mfalme wa Ulimwengu ni changamoto kwa waamini kutafakari tena fadhila za Kimungu na Kibinadamu na kuona kama kweli wanashiriki kikamilifu katika ujenzi wa Ufalme wa Mungu, kwani hakuna haki pasi na amani na hakuna amani pasi na haki. RealAudioMP3

Fadhila ni msimamo wa kudumu tena imara unaomchangamotisha mwamini kutenda mema. Fadhila za kibinadamu ni hali thabiti, na maelekeo imara ya akili na ya utashi zinazotawala matendo ya binadamu, zinazoratibu harara na kuongoza mwenendo wa mwamini wa kufuata akili na imani. Fadhila hizi zinafumbatwa katika maisha adili, zinatakaswa na kuinuliwa na neema ya Mwenyezi Mungu.

Haki ni kati ya fadhila za binadamu; ni nia na utashi wa kudumu na imara wa kuwapa wengine wanachostahili. Haki kwa Mwenyezi Mungu inaitwa "fadhila ya dini". Yesu ni Mfalme wa Haki na Amani changamoto kwa kila mwamini kuhakikisha kwamba, anajenga na kudumisha utamaduni wa kutenda haki. Kila mtu anahamasishwa kuwa ni mdau wa Haki Jamii, ukweli na uwazi! Mama Kanisa anapohitimisha Mwaka wa Imani, anawaalika waamini kuendelea kuombea misingi ya haki na amani anasema Askofu mkuu Lebulu.

Imani ni fadhila ya Kimungu ambayo kwayo mwamini anamsadiki Mwenyezi Mungu na kila kitu ambacho amekifunua na Kanisa linawataka waamini kusadiki, kwani Mungu ndiye utimilifu wa ukweli wenyewe. Mwanadamu anapaswa kufahamu na kutekeleza mapenzi ya Mungu katika maisha yake, kwani imani hutenda kazi kwa upendo. Ufalme wa Kristo unafumbatwa katika imani na utakatifu wa maisha.

Askofu mkuu Josephat Lebulu katika tafakari kuhusu Sherehe za Kristo Mfalme anahitimisha kwa kusema kwamba, amani na imani ni chanda na pete, ndiyo maana kuna haja ya kusimama kidete kulinda na kutetea uhuru wa kuabudu, kwani huu ni msingi wa haki nyingine zote za binadamu.







All the contents on this site are copyrighted ©.