2013-11-22 10:09:26

Mafundisho Jamii ya Kanisa ni nguzo ya haki jamii inayodumisha: utu na heshima ya binadamu


Mafundisho Jamii ya Kanisa ni utajiri mkubwa unaofundishwa na Mama Kanisa katika masuala yanayogusa usawa na utofauti katika maisha ya mwanadamu kama njia ya kuonesha mshikamano wa dhati katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Watu wanapaswa kutambua na kuthamini tofauti zinazojitokeza katika maisha yao sanjari na kutambua umuhimu wake katika utandawazi na kwamba, kila mtu anayo nafasi ya pekee katika Jamii inayomzunguka. Vijana wanaonesha jeuri na nguvu ya kusonga mbele kwa matumaini na ari kuu zaidi, wakati ambapo wazee ni hazina ya hekima na busara; kumbe, wanapaswa kutegemezana kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Jamii husika.

Vijana wasiokuwa na ajira ambao ni asilimia kubwa katika jamii ni janga la kimataifa kwa siku za usoni. Ni watu wasiokuwa na matumaini kwa leo na kesho iliyo bora zaidi, jambo linalohatarisha amani na usalama kwa Jumuiya ya Kimataifa. Hii ni sehemu ya ujumbe uliotolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwa washiriki wa Tamasha la tatu la Imani, lililofanyika mjini Verona, Alhamisi, tarehe 21 Novemba 2013.

Baba Mtakatifu anasema, Mafundisho Jamii ya Kanisa ni rejea katika medani mbali mbali za maisha kama sehemu ya mchakato wa waamini walei kuyatakatifuza malimwengu badala ya kuwa na uchu wa mali na madaraka pamoja na baadhi ya watu kutafuta faida kubwa. Mafundisho Jamii ya Kanisa yanayosheheni tafakari za Imani yanapania kuwajengea waamini na watu wenye mapenzi mema uhuru wa ndani na dhamiri nyofu, daima wakitoa kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu; wakijitahidi kuongozwa na kanuni auni, ili kujenga na kudumisha matumaini kwa wale waliokata tamaa.

Baba Mtakatifu anasema Mafundisho Jamii ya Kanisa yanapania kujenga na kudumisha haki jamii, maendeleo endelevu ya watu pamoja na kushiriki katika mchakato wa kutengeneza fursa za ajira kwa kuondoa mambo yote yanayokwamisha utekelezaji wa haki jamii.

Ni mafundisho yanayokazia mshikamano wa kidugu baina ya watu wa mataifa. Mshikamano kwa wachumi ni jambo linaloonekana kuwa kama fedheha. Watu wajenge na kuimarisha mshikamano na ushirikiano kama njia ya kupambana na changamoto mbali mbali za maisha mintarafu usawa na utofauti. Waamini na watu wenye mapenzi mema, hawana budi kujielekeza katika kukuza na kudumisha moyo wa mshikamano na ushirikiano katika kukabiliana na majanga ya maisha; kwa kushuhudia imani katika matendo.







All the contents on this site are copyrighted ©.