2013-11-22 11:57:13

Jitahidini kumwabudu Mungu kwa ibada, usikivu, tafakari, toba na wongofu wa ndani, ili kupokea msamaha na upendo wa Mungu!


Hekalu ni mahali patakatifu panapotumiwa na waamini kwa ajili ya kumwabudu, kumshukuru na kumtukuza Mwenyezi Mungu. Mwili wa binadamu ni hekalu la Fumbo la Utatu Mtakatifu, mwaliko kwa waamini kumsikiliza Mwenyezi Mungu anayezungumza kutoka katika undani wa maisha yao; tayari kufanya toba na kuomba msamaha ili kuendelea kumfuasa Mwenyezi Mungu kwa njia ya Kristo.

Hekalu ni mahali pa rejea kwa waamini na Jamii husika kama ilivyokuwa kwenye Agano la Kale. Jambo muhimu linalotekelezwa ndani ya Hekalu au Kanisa si nyimbo au ibada inayofanyika humo, bali ni mkusanyiko wa Familia ya Mungu inayoungana kuadhimisha Sadaka ya Misa Takatifu pamoja na kumwabudu Mwenyezi Mungu, ambaye ndiye kiini rejea cha uwepo wa Kanisa au Hekalu.

Waamini wajibidishe kumwabudu Mungu kutoka katika undani wa maisha yao kwa kuthamini utakatifu wa maisha ya imani. Kamwe waamini wasimhuzunishe Roho Mtakatifu waliyempokea kwa Sakramenti ya Ubatizo na Kipaimara. Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko Ijumaa tarehe 22 Novemba 2013 kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kuendelea kujitakatifuza kwa kutambua kwamba, kama binadamu wanaandamwa na dhambi. Mwamini anaweza kuboresha na kuyatakatifuza maisha yake kwa njia ya sala, toba na wongofu wa ndani, ili kuonja huruma na upendo wa Mungu unaotolewa kwa njia ya sakramenti ya Upatanisho na kuimarishwa na Sakramenti ya Ekaristi Takatifu.

Kwa njia hii, waamini wanaweza kumwabudu Mwenyezi Mungu kutoka katika undani wa maisha yao: kwa ibada, usikivu na tafakari ya Neno la Mungu; kwa toba na wongofu wa ndani; kwa kuomba na kupokea msamaha, ambao ni wimbo wa sifa kwa Mwenyezi Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.