Jengeni umoja na mshikamano Afrika, msikubali kugawanya na kubebeshwa kinzani!
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amewataka mawaziri
na maofisa waandamizi wa nchi za Afrika wanaoshiriki katika majadiliano na nchi zilizoendelea
kutafuta njia za kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi kukataa kufarakanishwa
ama kugawanywa na nchi tajiri.
Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa suala la nchi
tajiri kuzisaidia nchi zinazoendelea kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia
nchi siyo hisani wala fadhila bali ni wajibu wa nchi hizo tajiri ambazo kimsingi ndio
wamesababisha matatizo makubwa ya tabia nchi ambayo dunia inakabiliana nayo.
Rais
Kikwete ameyasema hayo Alhamisi, Novemba 21, 2013, wakati alipohutubia mawaziri wanaounda
Umoja wa Mawaziri wa Afrika kuhusu Mazingira – African Ministerial Conference on Environment
(AMCEN) pamoja na Kundi la Maofisa Waandamizi wa Afrika Wanaoshiriki katika Majadiliano
kuhusu Mabadiliko ya Tabia Nchi – African Group of Negotiators (AGN) ikiwa ni sehemu
ya Mkutano wa Kimataifa wa Mabadiliko ya Tabia Nchi – COP19/CMP9, unaoendelea kwenye
Uwanja wa Taifa wa Michezo wa Poland mjini Warsaw.
Rais Kikwete anahudhuria
Mkutano huo wa siku tatu, akiwakilisha Bara la Afrika katika nafasi yake ya Uenyekiti
wa Kamati ya Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Mazingira (CAHOSCC), nafasi ambayo aliombwa
na viongozi wenzake aitumikie mwanzoni mwa mwaka huu. Ataishikilia nafasi hiyo kwa
miaka miwili.
Akizungumza na mawaziri hao, Rais Kikwete amesema kuwa ni muhimu
kwa Afrika kushiriki katika majadiliano hayo ikiwa na sauti moja, wakikataa kugawanywa
ama kufarakanishwa kama namna ya kuwapunguza nguvu katika majadiliano hayo magumu
na ambayo bila shaka yanachukua muda mrefu. “Nimekuja hapa kuwaungeni mkono. Hii ni
sawa na vita na nyie ndio askari wa mstari wa mbele. Mimi ni Mkuu wa Majeshi ambaye
nimekuja kuwatembeleeni na kuwaunga mkono katika vita hii ngumu ya kuikoa dunia. Kwetu
sisi Waafrika, ushahidi wa mabadiliko ya tabia nchi uko wazi kabisa. Leo, tunapata
mafuriko hata katika Somalia, tokea lini tukapata mafuriko makubwa ya kiasi hiki jangwani?
Huwezi kujua, siku nyingine itakuwa ni Dar es Salaam ama Mombasa.”
Ameongeza
Rais Kikwete: “Ujumbe wangu ni ujumbe wa umoja, kuweni wamoja, msikubali kugawanywa,
wala kufarakanishwa kwa njia yoyote ile. Mimi kazi yangu ni kuwatakia mafanikio katika
mapambano haya. Tunachokitaka sisi katika Afrika tunakijua, uwezo wa kukitafuta tunao,
mnajua tulikotoka na mnajua tunakokwenda. Nawaamini sana, naamini katika uwezo wenu.”
Kuhusu
uamuzi wa Mikutano iliyopita wa nchi tajiri na zilizoendelea duniani kuzisaidia nchi
masikini zaidi duniani kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi, Rais Kikwete
amewaambia mawaziri hao: “Hili siyo suala la hisani wala fadhila. Huu ni wajibu wao
kwa sababu wao ndiyo wameifikisha dunia kwenye vurugu hii ya hatari. Hivyo, ni lazima
wabebe wajibu na jukumu la kutusaidia sisi masikini kukabiliana na hali hiyo kwa sababu
athari hizo zitamfikia kila mtu na kila nchi hata kama zitaanza kwa sisi tusiokuwa
na uwezo mkubwa.”
“Sisi ni kama Sungura aliyekutwa amebeba mishale na upinde
akiwa njiani kwenda kupambana na Tembo. Kila mtu alimcheka. Sisi ni kama Sungura anayekwenda
kupambana na Tembo. Kazi yetu ngumu kweli lakini siku moja, mahali fulani, Tembo ataanguka,”
alisema Rais Kikwete huku mawaziri hao wakiangua kicheko.
Mara baada ya kumaliza,
mazungumzo hayo ya Rais Kikwete yameungwa mkono na mawaziri kutoka nchi za Senegal,
Gabon, Uganda, Niger na Angola pamoja na Kamishna wa Maendeleo ya Vijijini na Kilimo
wa Umoja wa Afrika (AU) Mama Rhoda Peace Tumusiime.