2013-11-22 08:12:12

Jengeni moyo, ari, bidii na udumifu katika sala, ili kuweza kushuhudia imani katika matendo adili!


Askofu msaidizi Eusebius Nzigilwa, Mwenyekiti wa Idara ya Katekesi Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano na Radio Vatican wakati huu Mama Kanisa anapofunga Mwaka wa Imani, anawaalika waamini kujenga na kudumisha moyo wa sala katika maisha yao na kwamba, sala ni kwa ajili ya Familia nzima ya Mungu na wala hakuna upendeleo! RealAudioMP3

Anasema, Sala inamwezesha mwamini kuinua moyo wake kwa Mwenyezi Mungu, kwa kumwomba mema yanaylingana na matakwa yake. Hii daima ni zawadi safi kutoka kwa Mwenyezi Mungu anayekuja kukutana na mja wake katika undani wake wa maisha. Sala ya Kikristo ni fungamanisho hai na Fumbo la Utatu Mtakatifu.

Askofu msaidizi Nzigilwa anakiri kwamba, ingawa sala ni muhimu sana katika maisha ya mwamini, lakini waamini wengi bado hawajajenga ari, moyo, bidii na udumifu katika maisha ya sala na matokeo yake wanajikuta wakiogelea katika visingizio vinavyowakwamisha kupata nafasi na muda wa kusali kwa dhati. Kusali kunamwezesha mwamini kufunguliwa mifereji ya neema na baraka katika maisha yake.

Kumbe, Maadhimisho ya Mwaka wa Imani iwe ni kursa ya kukuza na kuimarisha ari na moyo wa kupenda kusali zaidi, ili kupata nguvu ya kumshuhudia Mungu katika Imani, Liturujia na Sakramenti za Kanisa, katika maisha adili na matakatifu na hatimaye, kuifanya sala kuwa ni kielelezo cha imani tendaji.







All the contents on this site are copyrighted ©.