2013-11-21 09:33:27

Siku ya Wavuvi Duniani kwa Mwaka 2013


Jumuiya ya Kimataifa kila mwaka ifikapo tarehe 21 Novemba, inaadhimisha Siku ya Wavuvi Duniani. Lengo ni kuwaenzi wavuvi wanaotekeleza wajibu wao katika mazingira magumu na hatarishi na kwamba, wanachangamotishwa kuwa makini katika matumizi ya rasilimali iliyoko majini, ili iweze kuwa ni kwa mafao ya wengi.

Sekta ya uvuvi nchini Ufilippini imeathirika kwa kiasi kikubwa baada ya kukumbwa na tufani iliyopelekea maafa makubwa ya maisha na mali za watu. Hii ni Jamii inayohitaji kuonjeshwa mshikamano wa upendo na ukarimu, ili iweze kuanza tena maisha kwa matumaini pasi na kukata tamaa!

Baraza la Kipapa la wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum katika ujumbe wake kwa Maadhimisho ya Siku ya Wavuvi Kimataifa, linasema, nyakati hizi dunia inaendelea kushuhudia mashindano ya kutafuta faida kubwa, hali ambayo imepelekea wavuvi wengi kufanya kazi katika mazingira magumu na hatarishi, hali inayosababisha ajali za mara kwa mara na kwamba, wavuvi ni Jamii ya watu ambao kwa sehemu kubwa haina hifadhi za kijamii.

Wavuvi wengi wanafanya kazi bila ya kuwa na mikataba ya kazi; wanapewa misharaha "kiduchu" ambayo haikidhi mahitaji msingi ya wavuvi pamoja na familia zao. Ni Jamii inayofanya kazi kwa masaa mengi bila ya kukutana na kuonana na familia zao, hali ambayo inakwamisha malezi, ustawi na maendeleo ya familia nyingi za wavuvi. Sekta ya uvuvi inatoa ajira kwa wavuvi ambao hawana elimu kubwa na matokeo yake wanakosa sauti ya kudai haki zao msingi na hivyo daima wanajikuta wakiwa pembezoni mwa Jamii nyingi.

Katika ulimwengu wa utandawazi, Sekta ya Uvuvi imejikuta ikikabiliana na ukosefu wa wafanyakazi, jambo ambalo limepelekea dhuluma, unyonyaji na unyanyasaji wa wavuvi, ambao wengi wao ni wale wanaopatikana kutokana na biashara haramu ya binadamu, wakimbizi na wahamiaji wanaotafuta nafuu na ubora wa maisha ughaibuni. Wavuvi wamekuwa pia wakishirikishwa katika biashara haramu ya binadamu kwa kutumia vyombo vyao vya uvuvi.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, alipokuwa anazungumza na washiriki wa Kongamano la la XXIII la Wavui Kimataifa, lililofanyika mjini Vatican kunako mwaka 2012, aliwataka wavuvi kuhakikisha kwamba, wanalinda utu na heshima yao; wazingatie usalama kazini; walinde na kudumisha tunu msingi za maisha ya kifamilia; sanjari na kusimama kidete kulinda na kutunza mazingira, daima wakiwa mstari wa mbele kutetea utu na heshima ya kila binadamu na kwamba, daima Kanisa liko pamoja nao!

Utume wa bahari unapenda kuwa ni sauti ya wale wasiokuwa na sauti kwa kufichua matatizo na hali ngumu wanayokabiliana nayo wavuvi wanapokuwa kazini pamoja na changamoto zinazozikumba familia zao wanapokuwa mbali na makazi yao. Jumuiya ya Kimataifa haina budi kuhakikisha kwamba, wavuvi wanakuwa na mazingira bora na salama ya kazi; wanapata tiba, matibabu na muda wa kutosha kwa ajili ya mapumziko; mikataba ya kazi pamoja na hifadhi za kijamii kama ilivyo kwa wafanyakazi kutoka katika sekta mbali mbali za kiuchumi na kijamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.