Nchi tajiri zitekeleze ahadi yake katika mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi!
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amezitaka nchi tajiri
na zilizoendelea duniani kutimiza ahadi zao za kutoa fedha kusaidia nchi masikini
zinazoendelea kuchukua hatua za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi.
Amesema
kuwa rekodi zinaonyesha kuwa nchi tajiri na zilizoendelea hazijatoa fedha zozote mpya
kwa ajili ya kugharimia hatua za kupambana na athari za mabadiliko ya tabia nchi katika
miaka mitatu iliyopita, kama ilivyokubaliwa, na badala yake nchi tajiri zimekuwa zinatoa
fedha ambazo ziliahidiwa siku nyingi.
Aidha, Rais Kikwete ametaka kuwepo kwa
uwazi kuhusu jinsi ahadi hizo zinavyotimizwa na jinsi fedha inavyogawanywa duniani
kwa sababu mpaka sasa kuna ukosefu mkubwa wa uwazi katika jambo hilo.
Rais
Kikwete amesema hayo Jumatano, Novemba 20, 2013, wakati aliposhirikiana na Katibu
Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mheshimiwa Ban Ki Moon kufungua Mjadala wa Mawaziri kuhusu
Jinsi ya Kugharimia Hatua za Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabia Nchi ikiwa ni sehemu
ya Mkutano wa Kimataifa wa Mabadiliko ya Tabia Nchi (COP19/CMP9) unaoendelea mjini
Warsaw, Poland.
Akishiriki katika ufunguzi wa Mjadala huo kwenye Uwanja wa
Taifa wa Poland ambako Mkutano wa Tabia Nchi unafanyika, Rais Kikwete amewaambia wajumbe
kuwa jitihada za nchi zinazoendelea kukabiliana na athari za mabadiliko ya taiba nchi
zinakwamishwa na ukosefu wa fedha zilizoahidiwa na nchi zilizoendelea. “Kama mnavyokumbuka,
mwaka 2010 mjini Cancun, Mexico, Jumuia ya Kimataifa ilielewa hali ya nchi zinazoendelea
na kukubali kugharimia hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi. Yalikuwa
ni makubaliano yaliyotoa kipaumbele kwa nchi masikini zaidi duniani (LDC’s), yaani
Mataifa Madogo ya Visiwa na Afrika,” amesema Rais Kikwete na kuongeza:
“Ahadi
ya pesa mpya na ya nyongeza ya kiasi cha dola za Marekani bilioni 30 ilileta matumaini
mapya katika mazingira ya kukatisha tamaa kwa nchi walengwa. Lakini sasa tunashuhudia
kuwa mambo hayakwenda kama ilivyokubaliwa. Kwanza, kiasi kikubwa kilichotolewa hakikuwa
fedha mpya wala za nyongeza, kama ilivyokubaliwa mjini Cancun.”
Rais Kikwete
amesema kuwa nchi chache ambazo zimetimiza ahadi yao zimefanya hivyo siyo kwa kutoa
fedha mpya wala za nyongeza isipokuwa kwa kutoa fedha za Misaada ya Maendeleo (ODA)
zilizokuwa zimeahidiwa huko nyuma.
“Isitoshe, sehemu kubwa ya fedha hizo zilitolewa
kwa nchi zenye kipato cha kati. Hii ilikuwa tofauti na makubaliano kuwa fedha zingeelekezwa
kwa mahitaji ya nchi masikini zaidi kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi.”
Rais
pia ametaka uwazi zaidi katika kutolewa kwa fedha hizo. “Hali ya ukosefu wa uwazi
inasababisha ugumu wa kujua kama ahadi zimetimizwa ama hazijatimizwa, na kama zimetimizwa
ni kwa namna gani. Isitoshe, hakuna uratibu wa utoaji wa fedha na mchakato wa kuweza
kupata fedha hizo ni mrefu na mgumu. Ukosefu wa utabiri huo unasababisha ugumu wa
kuamua faida za fedha za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi.”
Ameongeza
Rais Kikwete: “Njooni niwapeni mfano wa Tanzania ili kuthibitisha ninayoyasema. Tathimini
yetu ya karibuni inaonesha kuwa nchi yetu imepokea dola za Marekani milioni 20 kwa
ajili ya kuunga mkono masuala ya tabia nchi. Lakini rekodi za wafadhili zinaonyesha
kuwa kiasi kilichotolewa kwa Tanzania ni kikubwa mno – dola milioni 200. Ni jambo
la kushangaza sana kuwa tumeweza kurekodi asilimia 10 ya kiasi kilichopokelewa.”
Amesisitiza
Rais Kikwete: “Haya, kwa maoni yangu, ndiyo baadhi ya mambo ya msingi ambayo yanahitaji
hatua za haraka za Jumuia ya Kimataifa. Fedha kwa ajili ya mabadiliko ya tabia nchi
zinatakiwa kunufaisha watu wote.”