2013-11-20 08:06:59

Wasomi, tafuteni ukweli!


Chuo Kikuu cha Kipapa cha Laternano, hivi karibuni kimezindua rasmi Mwaka wa Masomo 2013- 2014, chini ya uongozi wa Baba Mtakatifu Francisko, tukio ambalo limezinduliwa na Kardinali Augustino Vallini, Makamu Askofu Jimbo kuu la Roma na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kipapa cha Laterano.

Kardinali Vallini ameitaka Jumuiya ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Kipapa cha Laterano, kufanya tafakari ya kina kuhusu matukio makuu ya historia ya Kanisa, yaliyoshuhudia kwa unyenyekevu mkuu Baba Mtakatifu Benedikto XVI aking’atuka kutoka madarakani kwa hiyari yake mwenyewe kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo.

Kuchaguliwa kwa Baba Mtakatifu Francisko, limekuwa ni tukio jingine ambalo limewaacha walimwengu wakiwa wameshika tama kwa mshangao mkubwa. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI ameacha urithi mkubwa ambao pamoja na mambo mengine ni changamoto ya kuutafuta ukweli. Hii ni dhamana nyeti kwa wasomi ndani na nje ya Kanisa; ni utume unaopaswa kuendelezwa na vyuo vikuu pamoja na taasisi za elimu ya juu zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa.

Wasomi wautafute ukweli katika medani mbali mbali za maisha na kuwajengea wanafunzi uwezo wa kuanzisha mchakato wa kutafuta ili waweze kupata ukweli katika hija ya maisha yao hapa duniani. Ili kufanikisha lengo hili kuna haja ya kuwa na uhuru wa ndani, unaoiwezesha akili kusafisha yale yasiokuwa na umuhimu katika maisha, kwa kuzingatia ukweli.

Baba Mtakatifu Francisko mara tu baada ya kuchaguliwa kuliongoza Kanisa, aliwataka Makardinali na Taifa la Mungu katika ujumla wake kuzingatia mambo makuu matatu: kutembea, kujenga na kuungama imani kwa Kristo na Kanisa lake. Hii ni dira makini kwa Jumuiya ya Wasomi kuizingatia.

Chuo Kikuu hakina budi kuendeleza mchakato kwa njia ya tafiti kwa ajili ya mafao ya wengi; kipindi cha masomo, iwe ni fursa kwa wanafunzi kujengeka: kiakili, kiutu na kimaadili, kwa kujenga na kukuza kiu ya kutafuta ukweli na kumuungama Yesu Kristo Mkombozi wa dunia kwa njia ya ushuhuda wa imani tendaji.

Askofu mkuu Enrico Covolo, Makamu mkuu wa Chuo Kikuu cha Kipapa cha Laterano anasema kwamba, mwaka wa masomo 2013- 2014 unajikita zaidi katika shughuli za kichungaji kwa wanafunzi wa Chuo kikuu cha Laterano. Lengo ni kujenga na kuimarisha Jumuiya ya Chuo Kikuu cha Kipapa cha Laterano. Utekelezaji wa mikakati hii unajikita katika masomo, hapo Majaalim wanapaswa kutekeleza utume wao kwa kusukumwa na mfano wa Kristo mchungaji mwema, ili kuwasaidia wanafunzi kuweka uwiano safi kati ya akili na imani.

Kardinali Zen Ze Kiun, Askofu mkuu mstaafu wa Jimbo kuu la Hong Kong, China akitoa mhadhara wake kwa kuzingatia mchango wa Kardinali Henry Newman, anaasema, Jaalim anapaswa kuwa ni mlezi na mchungaji anayetekeleza wajibu na utume wake kwa niaba ya Mama Kanisa. Wanapaswa kuwafahamu na kuwasaidia wanafunzi wao kufikia ukomavu wa kiakili na kiimani, tayari kushiriki katika kuchangia elimu waliyoipata kwa ajili ya ujenzi wa Ufalme wa Mungu. Wanawajibika kushirikisha hekima waliyokirimiwa na Mwenyezi Mungu kwa jirani zao.

Majaalim wajitahidi kuwa kati na kwa ajili ya wanafunzi wao kama alivyojitahidi Mtakatifu Don Bosco kwa vijana wake; kama alivyofanya Yesu miongoni mwa wafuasi wake. Jumuiya ya Chuo kikuu ni sehemu ya mchakato kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa kwa siku za usoni.

Kardinali Zen Ze Kiun anasema, uhuru wa kidini nchini China unazongwa mno kiasi kwamba, Kanisa Katoliki haliwezi kutekeleza vyema wajibu na dhamana yake katika majiundo ya wanafunzi. Sheria mpya iliyotungwa hivi karibuni, imeliondolea Kanisa uwezo wa kuongoza shule zake 300 na badala yake imeundwa Tume itakayowajibika moja kwa moja kwa Serikali. Chuo Kikuu cha Kipapa, kinatarajia tarehe 21 Novemba 2013 kutembelewa na Rais Giorgio Napolitano wa Italia.








All the contents on this site are copyrighted ©.