2013-11-20 07:33:48

Wanawake wana mchango mkubwa katika kukuza na kudumisha misingi ya amani, ikiwa kama watawezeshwa!


Mkutano mkuu wa kumi wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni uliohitimishwa hivi karibuni mjini Busan, Korea ya Kusini imekuwa ni fursa ya kuweza kuchambua maana na umuhimu wa amani katika kukuza na kumwendeleza mwanadamu: kiroho na kimwili. Wajumbe wamechambua maana ya amani ndani na nje ya Kanisa, wakiongozwa na kauli mbiu “Mungu wa uhai, tuongoze katika haki na amani”. RealAudioMP3

Baadhi ya wajumbe kutoka Afrika wamebainisha kwamba, kwa kuwawezesha wanawake katika masuala ya misingi ya haki na amani, waliweza kuchangia kwa kiasi kikubwa katika mchakato wa haki, amani na upatanisho nchini Liberia, iliyokuwa imemezwa na machafuko ya vita ya wenywe kwa wenyewe iliyosababisha majanga na madhara makubwa kwa wanachi wa Liberia.

Wajumbe wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni wameyataka Makanisa kuhakikisha kwamba, yanashiriki kikamilifu katika kuzuia, kuponya na kujenga misingi ya haki na amani na kamwe yasiwe ni watazamaji wakati wa migogoro, machafuko na vita katika Jamii husika. Katika mchakato kama huu, Makanisa yaoneshe dhamana yake kwa kusimama kidete kutetea misingi ya haki na amani, hata kama yatasigana na Serikali zilizoko madarakani, kwani kuunga mkono vitendo vya uvunjaji wa haki msingi za binadamu zinazofanywa wakati mwingine na Serikali husika ni kuwavunja moyo wananchi.

Makanisa yajihusishe katika mchakato wa haki, amani na upatanisho, ili Jamii ziweze kupata amani ya kweli inayopata chimbuko lake katika maisha ya mwanadamu, amani ambayo ni dumifu! Wajumbe wamesema kunako Mwaka 1953 Korea ya Kusini na Kaskazini zilitiliana sahihi mkataba wa amani, lakini tangu wakati huo, bado zimeendelea kuishi katika hali ya uhasama, chuki na wasi wasi wa kuweza kuzuka tena kwa vita.

Jumuiya ya Kimataifa ilishuhudia madhara makubwa ya matumizi ya silaha za kinyuklia wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia, lakini jambo la kushangaza ni kuona kwamba, bado kuna mashindano makubwa ya utengenezaji, usambazaji na ulimbikizaji wa silaha za mahangamizi.

Wajumbe wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni katika mkutano wao wamesema, silaha za kinyuklia haziwezi kamwe kuwa ni msingi wa amani mintarafu imani ya Kikristo. Wajumbe waliwakumbuka watu wote wanaoendelea kuathirika kutokana na matumizi ya silaha za maangamizi kutoka sehemu mbali bali za dunia.








All the contents on this site are copyrighted ©.