2013-11-20 08:19:30

Siku ya kuwaombea wamonaki kupambwa na uwepo wa Baba Mtakatifu Francisko


Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi tarehe 21 Novemba 2013 majira ya jioni anatarajiwa kuwatembelea na kusali na Wamonaki Wacamaldoli wa Mtakatifu Anthoni Abate, wanaoishi na kutekeleza utume wao mjini Roma. Itakuwa ni fursa kwa Baba Mtakatifu kusali pamoja na wamonaki hawa, kama sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Wamonaki, kama inavyojulikana kwa lugha ya Kilatini “Pro Orantibus”.

Ni siku ambayo Mama Kanisa anaitumia kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwaombea Wamonaki wanaojitosa kwa sala, sadaka na tafakari ya kina ya Neno la Mungu katika hija ya maisha yao. Siku kuu hii ilianzishwa kunako Mwaka 1953 na Papa Yohane wa Ishirini na tatu, aliyetangaza kwamba, Kanisa katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria kutolewa Hekaluni, liwakumbuke pia Wamonaki wanaojitoa bila ya kujibakiza kwa njia ya sala na tafakari ya kina kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake.

Lakini itakumbukwa kwamba, Siku kuu ya Bikira Maria kutolewa Hekaluni ilianzishwa na Papa Pio wa Kumi na mbili kunako tarehe 13 Mei 1953, siku maalum kwa ajili ya kusali na kuwaombea Wamonaki waliotawanyika sehemu mbali mbali za dunia sanjari na kuwasaidia kwa hali na mali ili waweze kuendeleza utume wao kwa Kristo na Kanisa lake. Hata kama miito ya maisha ya kuwekwa wakfu inachechemea, lakini bado watawa wanayo nafasi na dhamana kubwa katika maisha na utume wa Kanisa. Watawa wa ndani wana maisha tofauti kabisa, ni kundi linalopaswa kutiwa moyo.

Wamonaki wa Camaldoli wanajiandaa kumpokea na kumkaribisha Baba Mtakatifu Francisko anasema Mama mkuu Maria Michela Porcelato kwa furaha na moyo wa sala. Hili ni Shirika lililoanzishwa kunako Karne ya kumi na nane na Mama Angela Maria Pezza, mjane aliyekuwa na watoto watatu kwa kushirikiana na Watawa wa kiume Wacamaldoli wa Mtakatifu Gregori. Leo hii watawa hawa wanatekeleza utume wao nchini: Italia, Tanzania, Polandi, Brazil na India. Ni watawa wanaoipamba siku yao kwa sala, tafakari na kazi. Kuna kundi kubwa la waamini kutoka Jimbo kuu la Roma wanaofika kwenye Monasteri hii kwa ajili ya kupata ushauri wa maisha ya kiroho.








All the contents on this site are copyrighted ©.