2013-11-20 07:52:28

"Msipokuwa na imani thabiti mtatangatanga kama daladala iliyo katika usukani"!


Kardinali William Levada, Mwenyekiti mstaafu wa Baraza la Kipapa la Mafundisho tanzu ya Kanisa katika tafakari yake juu ya Mwaka wa Imani kama sehemu ya Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na Miaka 20 ya Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki anasema, ilikuwa ni hamu na utashi wa Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, kuona kwamba, Mwaka wa Imani unawasaidia waamini kusoma na kupitia tena Nyaraka za Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican pamoja na Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki, nyaraka muhimu sana katika mabadiliko ya maisha na utume wa Kanisa. RealAudioMP3

Mwenyeheri Yohane Paulo II alipokua anazungumza na Tume ya Makardinali waliokuwa wamepewa dhamana ya kuandika Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki aliwakumbusha kwamba, Katekisimu hii inapaswa kuwa ni chombo cha umoja na mshikamano katika imani; umoja ambao unapata chimbuko lake katika Fumbo la Utatu Mtakatifu. Katekisimu iwe ni muhtasari wa Imani, Sakramenti, Maisha Adili na Sala ya Kanisa. Iwe ni mwongozo katika katekesi zinazotolewa na Mabaraza ya Maaskofu Katoliki sehemu mbali mbali za dunia, kwa ajili ya Wakatekumeni.

Kardinali Levada anakumbusha kwamba, Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki ni Kitabu cgha rejea kwa Maaskofu waliopewa dhamana ya kufundisha imani, kuwaongozwa na kuwatakatifuza Watu wa Mungu katika hija ya maisha yao hapa duniani. Ni kitabu muhimu kwa wadau wa Uinjilishaji wanaomsaidia Askofu kutekeleza wajibu wake barabara. Hawa ni Makleri, Watawa, Makatekista na Walimu wa dini shuleni.

Ni chombo na mwongozo kwa wahubiri na kwa ajili ya waamini wote katika mchakato wa majiundo endelevu ya Familia ya Mungu; kielelezo cha utofauti katika umoja katika ujenzi wa Fumbo la Mwili wa Kristo yaani Kanisa. Hili ni Kanisa moja, Takatifu, Katoliki na la Mitume. Ni msingi wa utume na maisha ya viongozi wa Kanisa katika ujumla wao. Mama Kanisa anawahitaji waamini walei wanaoifahamu kwa kina na mapana imani: wanayoikiri kwa vinywa vyao; kuiadhimisha katika matendo ya Kiliturujia na Kisakramenti; Imani inayojidhihirisha katika matendo adili yanayoongozwa na Amri za Mungu; imani inayomwilishwa katika Sala na Matendo ya huruma.

Kumbe, ni dhamana ya Kanisa kuhakikisha kwamba, waamini wanafundishwa kikamilifu juu ya Imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, ili kuweza kuwa na waamini ambao wako tayari kujitosa kimasomaso kutolea ushuhuda wao kwa maneno, lakini zaidi kwa njia ya matendo yao! Waamini wasipokuwa na imani thabiti, wataendelea kutangaza tanga kama ”daladala” iliyokatika usukani. Watashindwa kuwa ni chumvi na mwanga wa dunia.

Ni mwaliko kwa Wakristo kuhakikisha kwamba, imani hii wanawarithisha pia watoto wao kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo, mlango na kitambulisho cha Mkristo. Sakramenti zimewekwa ili kuwatakatifuza wanadamu; kulijenga Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa na hatimaye, kumtolea Mwenyezi Mungu ibada. Hizi ni ishara zinazodai imani inayomwilishwa katika ushuhuda na matendo adili. Waamini wajitahidi kuifahamu Kanuni ya Imani kwa kichwa, kwani ni sehemu ya Uinjilishaji mpya na mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu.

Waamini waifahamu imani ya Kanisa na kuitolea ushuhuda; wawe na ujasiri wa kuitetea pale inaposhambuliwa. Huu ni mchakato wa Familia ya Mungu katika ujumla wake. Waamini wahakikishe kwamba, wana imarishwa kwa Sakramenti ya Kipaimara, tayari kuwa kweli ni Maaskari amini wa Kristo; wawe tayari kuwasha moto wa Injili kwa watu wenye kiu ya kusikia Neno la Mungu likitangazwa kwenye viunga na maeneo yao ya kujidai!

Na kwa makala hii, leo tunafunga mfululizo wa tafakari ya kina kuhusu Maadhimisho ya Mwaka wa Imani sanjari na Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na Miaka 20 tangu Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki ilipochapishwa. Ikumbukwe kwamba, kila mwaka ni mwaka wa imani, ndivyo Kardinali William Levada, Mwenyekiti mstaafu wa Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa anavyowatupia ”madongo” waamini katika Kufunga Mwaka wa Imani.

Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.