2013-11-20 14:45:24

Mapadre ambao kimsingi ni wahudumu wa Sakramenti ya Upatanisho wanahitaji kuonja upatanisho na uponyaji!


Baba Mtakatifu Francisko, wakati wa katekesi yake, Jumatano tarehe 20 Novemba 2013 kama sehemu ya mwendelezo wa tafakari juu ya Kanuni ya Imani amegusia kipengele cha "Ubatizo mmoja kwa maondoleo ya dhambi" na kuhusu "funguo" walizokabidhiwa Mitume kwa ajili ya maondoleo ya dhambi. Roho Mtakatifu aliyewashukia Mitume baada ya Ufufuko wa Kristo ndiye mhusika mkuu katika maondoleo ya dhambi na Kanisa likakabidhiwa dhamana hii kuitunza.

Baba Mtakatifu anafafanua kwamba, Kanisa ni mhudumu tu wa msamaha unaotolewa na Kristo kwa njia ya Roho Mtakatifu. Kanisa linawasindikiza waamini katika hija ya toba na wongofu wa ndani kwa maisha yao yote sanjari na kuwaalika kuonja tena mang'amuzi ya upatanisho wenye mwelekeo wa Kijumuiya na Kikanisa. Msamaha huu unatolewa kwa njia ya Padre.

Kwa njia ya utume wa Padre, Mwenyezi Mungu amewakirimia waamini ndugu anayeweza kuwapatia msamaha wa dhambi kwa njia ya Kanisa. Mapadre ambao kimsingi ni wahudumu wa Sakramenti ya Upatanisho watambue kwamba, hata wao wanahitaji kuonja huruma na uponyaji na kwamba, ni utume wanaopaswa kuutekeleza kwa njia ya unyenyekevu na huruma.

Baba Mtakatifu Francisko anawakumbusha waamini kwamba, kamwe Mwenyezi Mungu hawezi kuchoka kuwapatia msamaha. Anawaalika waamini kuthamini Sakramenti ya Upatanisho na kufurahia zawadi ya huruma na uponyaji inayopatikana kwa njia ya utume unaotolewa na Mapadre. Kwa njia hii, waamini wanaweza kutembea kwa uaminifu kama wafuasi wa Kristo.Amewaomba waamini na mahujaji kuendelea kusali kwa ajili yake na kwamba, Yeye pia anasali kwa ajili yao!

Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu ametambua uwepo wa Mapadre kutoka Polandi wanaotekeleza utume wao miongoni mwa wahamiaji na wakimbizi kutoka Poland. Anasema, wahamiaji wanakabiliana na changamoto mbali mbali katika maisha yao: wana wasi wasi mwingi, wanakabiliana na matatizo na hatari katika maisha na wakati mwingine wanajikuta kwamba, wanakata mizizi na tamaduni na hata familia zao.

Amewataka Mapadre hao kuwa mstari wa mbele ili kuwasaidia ndugu zao katika maisha ya kiroho, ili waweze kutunza imani na daima wakiwa mashahidi wa Jamii wanamoishi. Mwishoni, Baba Mtakatifu amewakumbuka kwa namna ya pekee wananchi wa Sardegna wanaokabiliana na mafuriko.







All the contents on this site are copyrighted ©.