2013-11-19 12:08:04

Wazee ni hazina ya Jamii, waheshimiwe na kutunzwa!


Jamii inapaswa kuwaheshimu na kuwaenzi wazee kwani hawa ni maktaba hai inayoiwezesha Jamii kurithisha tunu bora za maisha ya kiroho na kiutu; mapokeo na tamaduni njema kutoka kizazi kimoja hadi kingine kama alivyofanya Eliezari shahidi anayesimuliwa kwenye Kitabu cha Kwanza cha Wamakabayo.

Ni shahidi aliyethubu kukabiliana na kifo dini kuliko kudanganya kuhusu Sheria na Amri za Mungu, akalijitahidi kuwa mwaminifu kwa Mungu na Jamii hadi dakika ya mwisho wa maisha yake na wala vitisho vya kifo havikumtia wasi wasi, bali alitamani kuwaachia vijana urithi utakaodumu katika maisha yao! Alihisi dhamana kubwa iliyokuwa mbele yake kama Mzee katika Jamii na mfano wa kuigwa na vijana wa kizazi kipya katika imani na maisha adili. Ni mfano unaoweza kutolewa na mashahidi wa kila siku katika familia! Wazee waheshimiwe na kamwe si watu wa kubezwa na kutengwa!

Ni changamoto iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, Jumanne, tarehe 19 Novemba 2013 wakati wa Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, kilichoko mjini Vatican. Baba Mtakatifu anasema, wazee ni watu waliotangaza Habari Njema ya Wokovu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao, wakajitahidi kuwa waaminifu kwa Neno la Mungu na maisha adili. Inasikitisha kuona wazee wengi wakikabiliwa na magonjwa na hali ya kukata na kukatishwa tamaa. Ni wazee ambao wengi wao wametelekezwa kwenye nyumba za wazee na hospitalini, lakini ikumbukwe kwamba, wazee ni hazina ya Jamii.

Hawa ni mashahidi wa imani, waliovumilia madhulumu, wakawa tayari kurithisha imani yao kwa vijana wa kizazi kipya. Jambo la msingi ni Jamii kuendelea kuwa na huruma na mapendo kwa wazee, kwa kuwasikiliza na kuwahudumia kwa moyo mkuu na unyenyekevu.









All the contents on this site are copyrighted ©.