2013-11-19 08:40:25

Tarehe 24 Novemba 2013 Papa kukabidhi Waraka wa "Furaha ya Injili" kwa waamini kama sehemu ya kufunga Mwaka wa Imani


Baba Mtakatifu Francisko katika kilele cha Maadhimisho ya Mwaka wa Imani sanjari na Siku kuu ya Yesu Kristo Mfalme wa Ulimwengu anatarajiwa kuwakabidhi waamini Waraka Mpya wa Kichungaji, "Evangelii Gaudium" Yaani "Furaha ya Injili" kama alama ya kudumu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Ibada ya Misa inatarajiwa kuanza saa 4:30 kwa saa za Ulaya.

Hayo yamesemwa na Askofu mkuu Rino Fisichella, Rais wa Baraza la Kipapa la Uhamasishaji wa Uinjilishaji mpya alipokuwa anazungumza na vyombo vya habari mjini Vatican siku ya Jumatatu, tarehe 18 Novemba 2013. Mkutano huu umehudhuriwa pia na viongozi waandamizi kutoka Baraza hili.

Tukio la Baba Mtakatifu Francisko kuwakabidhi waamini Waraka Mpya wa Kichungaji ndicho kiini cha Maadhimisho ya Kufunga Mwaka wa Imani, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Wawakilishi 36 kutoka katika nchi 18, watapewa dhamana ya kutangaza yaliyomo kwenye Waraka wa Furaha ya Imani, kwa kutambua kwamba, kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo, wanapewa dhamana ya kutangaza Injili ya Kristo kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao hadi miisho ya dunia. Waraka huu watakabidhiwa: Askofu kutoka Lituania, Padre mmoja kutoka Tanzania na Shemasi kutoka Australia.

Baba Mtakatifu Francisko pia atawakabidhi Waraka huu Watawa wa Mashirika ya Kitawa na kazi za kichungaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia, walioshiriki kwa namna ya pekee kabisa kupamba Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, bila kuwasahau wasanii wanaoshiriki kikamilifu katika dhamana ya Uinjilishaji kwa njia ya karama na vipaji vyao. Kati ya waamini 36, wapo pia waandishi wa habari wawili watakaokabidhiwa dhamana ya kushiriki katika azma ya Utangazaji Injili, kwani Mama Kanisa anautambua mchango wao makini anasema Askofu mkuu Fisichella.

Waamini kwa mara ya kwanza katika historia ya Kanisa, wataweza kutoa heshima yao kwa masalia yanayosadikiwa kuwa ni ya Mtakatifu Petro, aliyeitwa kuwaimarisha ndugu zake katika imani, akasimama kidete kuitetea kwa njia ya ushuhuda wa maisha yake. Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani watu zaidi ya millioni 8. 5 wametembelea na kukiri Kanuni ya Imani kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.