Miradi ya umeme na maji yenye thamani ya zaidi ya sh bilioni 1.8 yazinduliwa Arumeru
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amezindua miradi ya maji na umeme wilayani Arumeru
yenye thamani ya zaidi ya sh. bilioni 1.8/- ikiwa ni utekelezaji wa mpango wa Serikali
wa Matokeo Makubwa Sasa (Big Results Now).
Amefanya uzinduzi huo Jumanne, Novemba
19, 2013 katika vijiji vya Chekereni na Manyire wilayani Arumeru, mkoani Arusha ikiwa
ni sehemu ya uzinduzi wa miradi kama hiyo katika mkoa mzima wa Arusha.
Akizungumza
na wakazi wa kijiji cha Chekereni, wilayani Arumeru, Waziri Mkuu alisema katika kutekeleza
mpango wa Matokeo Makubwa Sasa, Serikali imedhamiria kuvipatia maji safi vijiji 271
vya mkoa wa Arusha ifikapo mwaka 2014.
“Mwaka 2005, ni vijiji 121 tu kati ya
vijiji 342 vya mkoa huu ndiyo vilivyokuwa vikipata maji safi. Mwaka 2012 tulifikisha
vijiji 191, na jinsi tunavyokwenda tunataka tufikie vijiji 271 ifikapo mwaka 2014.
Kwa hiyo tutakuwa tumebakiwa na vijiji 71, na Mungu akijalia tunataraji kuwa ifikapo
mwaka 2015 tuwe tumevikamilisha vijiji vyote,” alisema huku akisangiliwa na mamia
ya wakazi waliojitokeza kushuhudia uzinduzi huo.
Aliwashukuru wadhamini wa
mradi huo wa Chekereni ambao ni kampuni ya Kiliflora kwa kugharimia ujenzi wa mradi
huo lakini akawataka wasiishie hapo bali waangalie zaidi namna ya kuwasaidia wananchi
wajiongezee fursa zao za kiuchumi.
Kwa upande wa mradi wa umeme, Waziri Mkuu
alimtaka mkandarasi aliyepewa kazi hiyo kuhakikisha kuwa anakamilisha mradi huo katika
muda muafaka na kwa kiwango cha juu.
“Hatutaki kusikia visingizio vya sababu
za hali ya hewa au sababu za kijiografia... Miradi hii ni ya gharama kubwa kwa hiyo
hatutaki visingizio. Meneja wa TANESCO hakikisha hakuna visingizio. Kama kazi hairidhishi,
ondoeni huyo mkandarasi, tafuta mwingine,” alisema.
Akisoma risala kuhusu mradi
wa maji wa Chekereni, Mhadisi wa Maji wa Halmashauri ya Wilaya ya Arusha, Bibi Joyce
Bahati alisema mradi huo ambao umegharimu sh. bilioni 1.15/-, utawanufaisha wakazi
wapatao 16,197 na kupunguza tatizo la maji katika vijiji vya Mlangarini, Moivaro Olkereian,
na maeneo jirani ya Kijenge.
“Mfuko wa Maendeleo wa Wafanyakazi wa shamba la
maua Kiliflora (KWDFL) umesaidia fedha na jamii imetoa nguvukazi pamoja na ardhi ya
ujenzi wa miundombinu,” alisema.
Alisema mradi huo ambao ulianza kutekelezwa
Septemba 2009, umehusiaha ujenzi wa kidaka maji; ujenzi wa matanki mawili yenye mita
za ujazo 90 kila moja; ujenzi wa vituo vya kuchotea maji 15 na utandazaji wa bomba
km 21 kutoka kwenye chanzo cha maji chemchem ya Songota.
Mapema akitoa taarifa
kuhusu mradi wa umeme vijijini (REA), Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Bw. George
Simbachawene alisema mradi wa kupeleka umeme vijini katika maeneo ya Manyire kupitia
Mlangarini, Seela Sambashamba, Timbolo, Ilkiding’a na Irkisongo wilayani Arumeru umegharimu
jumla ya sh. 631,440,000/- .
Aliitaja miradi mingine ya umeme vijijini inayofadhiliwa
na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ambayo pia inayotekelezwa na TANESCO kuwa ni:-
Mradi wa kupeleka umeme Halmashauri ya Wilaya ya Longido unaogharimu sh. bilioni
1.45/-; Mradi wa kupeleka umeme Mji wa Loliondo Wilaya ya Ngorongoro ambao gharama
yake ni sh. milioni 817/- na Mradi wa kupeleka umeme Vijiji vya Mto wa mbu Wilayani
Monduli ambao pia gharama yake ni sh. milioni 342/-.