2013-11-19 08:16:33

Je, bado waamini mna mwamko wa kutaka kujifunza Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki?


Kardinali William Levada, Mwenyekiti mstaafu wa Baraza la Kipapa la Mafundisho tanzu ya Kanisa katika tafakari yake juu ya Mwaka wa Imani kama sehemu ya Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na Miaka 20 ya Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki anasema kuna uhusiano wa dhati kati ya Mwaraka wa kichungaji: Mlango wa Imani na Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki. RealAudioMP3

Mwanzoni mwa Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican ilionekana kana kwamba, hakuna umuhimu wa kuwa na Katekisimu ya Kanisa Katoliki na kwamba, Nyaraka za Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican zilikuwa zinajitosheleza.

Lakini baadaye, waamini walikumbushwa kwamba, Mwenyezi Mungu alimpatia mwanadamu Amri kumi na wala si ushauri wa maisha ya kiroho na kimaadili, kumbe kulikuwa kuna haja ya kuwa na Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki na Muhtasari wa Mafundisho Jamii ya Kanisa: Hizi ni nyaraka zinazofundisha imani na maadili kwa kufumbata Maandiko Matakatifu na Liturujia ya Kanisa kwa ajili ya watu wa kizazi kipya.

Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, kunako Mwaka 1985 mara baada ya Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu akaamua kuufanyia kazi ushauri wa Mababa wa Sinodi kwa kuanzisha mchakato wa kutunga Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki, dhamana aliyopewa Kardinali Joseph Ratzinger kwa wakati huo. Akashirikiana na Tume ya Makardinali 12.

Katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolijia, ulimwengu unaonekana kuwa kama kijiji. Kumbe kutokana na changamoto hizi, kulikuwa na haja kwa Kanisa kuwa muundo wazi unaonesha umoja na mshikamano katika maisha ya kiroho kwa kuwa na: sheria za pamoja, Katekisimu kwa ajili ya Kanisa zima, Alama za Kiliturujia na mambo msingi katika shughuli za kichungaji.
Kardinali Levada anasema kwamba, Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki inasimikwa katika misingi mikuu minne ya maisha na utume wa Kanisa: Ni muhtasari wa imani inayoungamwa kwenye Kanuni ya Imani; Imani inayoadhimishwa kwenye Liturujia na Sakramenti za Kanisa; Imani inayomwilishwa katika uhalisia wa maisha kwa njia ya neema na Baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu mintarafu Amri kumi za Mungu na kwamba, hii ni imani inayowasukuma waamini kusali na kuimwilisha katika matendo ya huruma.

Kwa maneno mengine, Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki ni muhimu sana katika maisha ya Kanisa na utume wa Makatekista; ni chachu ya mageuzi na chombo cha kufundishia imani. Katekisimu ni muhtasari wa imani ya Kanisa iliyorithishwa kutoka katika Maandiko Matakatifu, ikafundishwa na Mababa wa Kanisa na Kumwilishwa na watakatifu pamoja na Wamissionari katika maisha na utume wa Kanisa sehemu mbali mbali za dunia.

Kwa hakika anasema Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki ni utajiri wa Kaniza zima. Katekisimu hii ilipotolewa kwa mara ya kwanza, watu wengi waliinunua. Je, baada ya miaka 20 tangu kuchapishwa kwake, waamini na watu wenye mapenzi mema bado wana ari na mwamko wa kutaka kujifunza yaliyomo kwenye Katekisimu hii?
Naam, usikose kujiunga nasi tena, tutakapoendelea kukuletea tafakari ya kina kutoka kwa Kardinali William Levada wakati huu Mama Kanisa anapofunga Mwaka wa Imani.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.