Askofu mkuu Zygmunt Zimowski, Rais wa Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa
wafanyakazi katika sekta ya afya anasema, kwamba, mkutano wa ishirini na nane wa Baraza
lake utakaoongozwa na kauli mbiu “Kanisa katika huduma kwa wazee wagonjwa: tiba kwa
wagonjwa walioathirika na magonjwa ya mishipa ya fahamu” ni mada inayopania kupembua
kwa kina na mapana athari zinazosababishwa na magonjwa haya katika karne ya ishirini
na moja.
Wataalam wa afya ya binadamu wanasema, haya ni kati ya magonjwa yanayoendelea
kusababisha vifo na mateso makubwa kwa wazee sehemu mbali mbali za dunia.
Mkutano
huu utakaohudhuriwa na wajumbe 400 kutoka sehemu mbali mbali za dunia, unatarajiwa
kufunguliwa kwa Ibada ya Misa Takatifu Alhamisi, tarehe 21 Novemba na kufungwa kwa
tafakari ya kina itakayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, hapo tarehe 23 Novemba
2013.
Askofu mkuu Zygmunt Zimowski anasema kwamba, mkutano huu unafanyika kwa
utashi ulioneshwa na Baba Mtakatifu Francisko, ili kuwasaidia wazee na watu wenye
umri mkubwa katika mchakato wa mapambano dhidi ya magonjwa sanjari na kuwapatia wazee
kipaumbele wanachostahili. Haki ya afya kwa wazee wagonjwa ni jambo la muhimu sana
katika Jamii pamoja na kuhakikisha kwamba, wazee wanapewa matunzo na heshima wanayostahili
kwa kushirikishwa katika maisha ya Jamii husika kadiri ya hali zao.
Wazee
ni hazina kubwa ya hekima na tunu bora za maisha ya kijamii, ikiwa kama watatumiwa
kikamilifu, lakini uzoefu unaonesha kwamba, wazee katika ulimwengu wa utandawazi na
maendeleo ya sayansi hawana nafasi tena, kwani wanaweka “kiwingu” kwa watu wengine
ndani ya Jamii kufurahia maisha.
Takwimu zinaonesha kwamba, duniani kuna zaidi
ya watu millioni 36 walioathirika kutokana na magonjwa ya mishipa ya fahamu kutokana
na uzee. Hadi kufikia mwaka 2050 inasadikiwa kwamba, idadi hii inaweza kuongezeka
maradufu, ikiwa kama Jumuiya ya Kimataifa haitachukua hatua za makusudi kupambana
na magonjwa ya mishipa ya fahamu yanayoendelea kusababisha mateso makali kwa wazee
na watu wenye umri mkubwa.
Huduma zinazotolewa kwa wagonjwa hawa Hospitalini
inaonekana kana kwamba, bado hazijaweza kufua dafu, anasema Askofu mkuu Zymowski,
hata katika nchi ambazo Serikali zimewekeza zaidi katika maboresho ya sekta ya afya.
Tija na ufanisi mkubwa vinaweza kupatikana kwa wagonjwa hawa kuhudumiwa katika maeneo
yao kwa kukazia kwanza kabisa: uchunguzi wa kina na tiba muafaka bila kusahau huduma
za kitabibu zinazopaswa kutolewa kwa wagonjwa kama hawa.
Wataalam, watafiti
na mabingwa wa magonjwa ya mishipa ya fahamu kutoka sehemu mbali mbali za dunia, kwa
muda wa siku tatu watakuwa mjini Vatican kubadilishana uzoefu na mang’amuzi katika
huduma kwa wazee wanaokabiliwa na magonjwa ya mishipa ya fahamu. Wajumbe watashirikisha
mikakati na sera makini zinazoweza kusaidia maboresho ya huduma ya afya kwa wagonjwa.
Itakumbukwa kwamba, Kanisa Katoliki liko mstari wa mbele katika huduma za
kiafya na wazee wamekuwa wakipatiwa huduma msingi kutoka katika taasisi zinazomilikiwa
na kuendeshwa na Kanisa, hapa wajumbe wataangalia taalimungu na mikakati ya kichungaji
kwa ajili ya wazee wagonjwa, ili kuwajengea imani, matumaini na mapendo, kwani hata
katika uzee na magonjwa yao, Kanisa bado linaendelea kuwathamini na linataka kuwaenzi.