2013-11-18 07:54:09

"Hakuna kulala hadi kieleweke!"


Kardinali William Levada, Mwenyekiti mstaafu wa Baraza la Kipapa la Mafundisho tanzu ya Kanisa anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuendeleza ari na mwamko wa maadhimisho ya Mwaka wa Imani, uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwani kila Mwaka unapaswa kuwa ni mwaka wa imani, “hakuna kulala hadi kieleweke”! RealAudioMP3

Anapenda kuchukua fursa hii kwa namna ya pekee kumshukuru Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita kwa kuwa na mwono mpana katika mikakati ya kichungaji, uliolihamasisha Kanisa kwa kupitia tena nyaraka za Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican pamoja na kukazia tena Katekisi makini na endelevu kama sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 20 tangu Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili alipoichapa kwa mara ya kwanza.

Kardinali Levada anasema kwamba, cheche za Maadhimisho ya Mwaka wa Imani ambao kwa sasa unaelekea ukingoni unapata chimbuko lake katika tafakari za wafanyakazi wa Baraza la Kipapa la Mafundisho tanzu ya Kanisa, walipoona umuhimu wa kufanya tena rejea ya kina kuhusu Mafundisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na miaka 20 ya Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki, matunda na changamoto ya Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, akashirikishwa wazo hili, akalikubali na kuridhia kuitisha Mwaka wa Imani. Maandalizi yakaanza mara moja, kwa kuchapisha mwongozo wa kichungaji kwa ajili ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani na baadaye Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, akachapisha Waraka wa kichungaji, “Porta Fidei” Mlango wa Imani.

Kardinali Levada anabainisha kwamba, kuna uhusiano mkubwa kati ya Uinjilishaji, Katekesi na Mwaka wa Imani. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, anabainisha mambo makuu mawili katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani kwamba, utume wa Kanisa unafumbatwa katika Katekesi makini na endelevu pamoja na Uinjilishaji, mwaliko kwa waamini kuhakikisha kwamba, wanajenga na kuimarisha uhusiano wao na Kristo, kwa kumpenda na kuwaonjesha jirani zao upendo na huruma inayobubujika katika imani yao kwa Kristo na Kanisa lake.

Waamini wanachangamotishwa na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika ujenzi wa Ufalme wa Mungu, utume ambao umetekelezwa na umati wa wamissionari kutoka sehemu mbali mbali za dunia, waliothubutu kujitosa kimasomaso kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake. Wamissionari hawa wakakumbana na vizingiti, changamoto na kinzani, lakini kamwe hawakukata tama na leo hii Kanisa limeenea sehemu mbali mbali za dunia.

Papa Paulo wa sita, aliwahi kusema kwamba, Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican uliochapisha nyaraka kumi na sita ni Katekesi ya kina na endelevu kwa watu wanaoishi katika ulimwengu mamboleo, changamoto na mwaliko kwa Mama Kanisa kusoma alama za nyakati, ili kujibu kwa uhakika kilio na hamu ya mioyo ya watu katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, ili Injili ya Kristo iendelee kuwa na mguso na mashiko katika maisha na vipaumbele vya watu.

Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walipania kufanya mabadiliko makubwa kwa kuleta hewa safi katika maisha na utume wa Kanisa; kwa kubadilisha mifumo iliyokuwa imepitwa na wakati. Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki ni mchango wa pekee kabisa uliotolewa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, tangu Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Kardinali levada anasema, Waraka wa kichungaji wa Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, Mlango wa Imani una utajiri mkubwa katika hija ya maisha ya kiroho na rejea kwa waamini katika maisha yao ya kila siku. Ni mlango unaowaowafungulia waamini mahusiano ya dhati na Mwenyezi Mungu kwa kusikiliza Neno la Mungu linalotangazwa na kuadhimishwa, tayari kumwilishwa katika uhalisia wa maisha.

Sakramenti ya Ubatizo ni cheti cha utambulisho wa Mkristo kama anavyosema Baba Mtakatifu Francisko, inayomwingiza mwamini katika Fumbo la Pasaka, yaani: mateso, kifo na ufufuko wa Kristo. Hapa mwamini anapata fursa ya kujenga na kuimarisha Familia ya Mungu inayotumwa kutangaza na kujenga Ufalme wa Mungu kwa njia ya ushuhuda wa imani tendaji. Fumbo la Pasaka, liliwasukuma Wamissionari wengi kujitosa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake. Fumbo la Pasaka ni zawadi inayowajibisha na kuendelea kuwachangamotisha waamini kutolea ushuhuda wa imani tendaji katika medani mbali mbali za maisha.

Kardinali Levada anabainisha kwamba, kumong’onyoka kwa tunu msingi za: imani, maadili na utu wema ni kati ya mambo yaliyopelekea kuitishwa kwa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, ili kuangalia jinsi ambavyo Kanisa linaweza kusaidia kumwilisha Habari Njema ya Wokovu kwa watu wa nyakati hizi. Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walitaka kuhakikisha kwamba, mafundisho tanzu ya Kanisa yanalindwa na kufundishwa kwa ufasaha, kwani ni mafundisho yanayomkumbatia mtu mzima: kiroho na kimwili.

Nyaraka za Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican bado ni Katekesi endelevu kwa maisha na utume wa Kanisa katika ulimwengu mamboleo pia ni chachu ya mageuzi ndani ya Kanisa.

Usikose kujiunga nasi tena, tutakapoendelea kukujuza kwa muhtasari tu: kuhusu Mlango wa Imani na Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.