Baba Mtakatifu atoa dawa ya maisha ya kiroho kwa waamini na mahujaji mjini Vatican
Jumapili iliyopita tarehe 17 Novemba 2013 wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, kwenye
Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, waamini na mahujaji waliokusanyika ili kuungana
na Baba Mtakatifu Francisko kwa Tafakari na Sala ya Mchana, walipewa tiba ya maisha
ya kiroho, itakayowasaidia katika kumwilisha mafanikio ya Mwaka wa Imani.
Hizi
ni juhudi zilizofanywa na Askofu mkuu Konrad Krajevski, mtunzaji mkuu wa Sadaka ya
Papa mjini Vatican, kwa kuwagawia waamini Rozari Takatifu na Picha ya Huruma ya Mungu,
inayoonesha matumizi sahihi ya dawa hii ya maisha ya kiroho katika hija ya waamini
kuyataktifuza malimwengu. Dawa hii imefungwa kitaalam kama Wafamasia wanavyofunga
dawa kwa ajili ya matumizi ya binadamu, hali inayoonesha kipaji cha ugunduzi hata
katika mambo ya kiroho.
Vifurushi vya dawa ya maisha ya kiroho vimeandaliwa
katika lugha mbali mbali, kati ya lugha hizi ni Kiingereza, Kiitaliani, Kihispania
na Kipolandi. Kwa hakika, watu wengi waliguswa na ugunduzi huu, kiasi cha kubaki wamepigwa
na bumbuwazi!