2013-11-16 08:22:31

Utume wa Bahari wachangia dolla za Kimarekani 10,000 kwa ajili ya wahanga wa majanga nchini Ufilippini


Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum, linawashukuru waamini na watu wenye mapenzi mema, ambao wanaendelea kuchangia kwa hali na mali katika kuokoa maisha ya watu wengi wanaoteseka nchini Ufilippini kutokana na kukumbwa na tufani ya Haiyan ambayo imesababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao. watu wengi wamepoteza maisha na mamillioni ya watu hadi sasa hayana makazi ya kudumu.

Baraza la Kipapa kwa namna ya pekee, linapenda kuwakumbuka mabaharia ambao wako kazini na hawana habari kuhusu hatima ya ndugu, jamaa na marafiki zao nchini Ufilippini. Wanawashukuru wote wanaowawezesha mabaharia hawa kuwasiliana na ndugu zao kwa njia ya simu pamoja na kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kama kielelezo cha mshikamano wa kiroho na waathirika nchini Ufilippini.

Kitengo cha Utume wa Bahari kutoka Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum, linachangia kiasi cha dolla za Kimarekani 10, 000 kusaidia juhudi za ujenzi mpya wa Ufilippini kwa kushirikiana na idara za utume wa Bahari nchini Ufilippini, ili kuwawezesha wananchi kuanza tena maisha yao ya kawaida licha ya magumu wanayokabiliana nayo!








All the contents on this site are copyrighted ©.