2013-11-16 09:05:11

Tamko la hija na kongamano la Mwaka wa Imani toka kwa Familia ya Mungu nchini Tanzania


Maadhimisho ya Mwaka wa Imani nchini Tanzania yamefikia kilele chake hapo tarehe 10 Novemba 2013 kwenye Parokia ya Bagamoyo, Jimbo Katoliki Morogoro, mahali ambapo ni Mlango na Mwanga wa Matumaini ya Kanisa Katoliki Tanzania. Kilele cha Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, kilitanguliwa na Kongamano la Siku mbili kwa ajili ya Familia ya Mungu nchini Tanzania. Lifuatalo ni tamko rasmi la hija na kongamano la Mwaka wa Imani lililotolewa na Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania.

1.0 UTANGULIZI
Mwaka 2012, Baba Mtakatifu Benedikto wa XVI alitangaza rasmi Mwaka wa IMANI. Kutokana na Tamko hilo, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), liliazimia kufanya shughuli mbalimbali ili kuchochea IMANI ya Waamini inayokabiliwa na changamoto zinazoelekea kutawala zaidi katika nyakati zetu na kuathiri IMANI kwa ujumla.

Ili kutekeleza azma hiyo, Baraza liliagiza kuwe na shughuli mbalimbali zinazolenga kuchochea IMANI miongoni mwa waamini katika ngazi mbalimbali: JNNK, Parokia, Jimbo na Kitaifa. Katika ngazi zote hizi kumekuwa na shughuli mbalimbali ikiwemo hija, semina, makongamano, na mafunzo mbalimbali yaliyowalenga maaskofu, mapadri, watawa wa kike na kiume, watoto, vijana, walei na waamini kwa ujumla.

2.0 LENGO LA MAADHIMISHO YA MWAKA WA IMANI.
Lengo la maadhimisho ya mwaka wa IMANI ni kutekeleza wito wa Baba Mt. Benedikto wa XVI unaohimiza uinjilishaji mpya kwa ajili ya kueneza IMANI ya Kikristo. Hii ikiwa ni fursa kamili ya kuliingiza Kanisa zima katika kipindi cha tafakari na ugunduzi wa IMANI ili kukabiliana na changamoto mbalimbali za kiimani.

3.0 CHANGAMOTO ZA KIIMANI
Baadhi ya changamoto za kiimani ni kama zifuatazo:
    Wakristo kutawaliwa na malimwengu
    Mabadiliko makubwa na ya haraka yanayofanya wakristo wazue au wapaswe kukabili maswali mengi kuhusu maisha na IMANI yetu.
    Uadui na upinzani unaojitokeza katika nyanja mabalimbali dhidi ya IMANI na maadili ya Kikristo
    Kiu na njaa ya watu wa zama hizi ya kutaka kukutana na Kristo na kufungamana naye.
    Uhitaji wa ushuhuda thabiti wa IMANI ya Kikristo.


4.0 HIJA NA KONGAMANO LA KITAIFA LA MAADHIMISHO YA KILELE CHA MWAKA WA IMANI.
Kongamano la Kitaifa la maadhimisho ya kilele cha mwaka wa IMANI limefanyika tarehe 8 - 10/11/2013 katika Kituo cha Hija cha Kitaifa, Bagamoyo, Jimbo Katoliki la Morogoro. Jumla ya washiriki wa kongamano hili ni waamini 1,131 wakiwemo Wahashamu Maaskofu 28, Abate 2, Mapadri 79, Watawa wasio makleri 183, Walei 310, Vijana 244 na Watoto 285.

Wakati wa maadhimisho haya, shughuli mbalimbali zimefanyika ikiwemo:
    Misa Takatifu,
    Uwasilishaji wa mada mbalimbali,
    Kupanda mti wa IMANI kwa kila Jimbo,
    Kuzindua mnara wa kumbukumbu wa mwaka wa IMANI Kitaifa,
    Hija ya Mwaka wa Imani,
    Burudani


Mada mbalimbali ziliwasilishwa na kujadiliwa katika vikundi vifuatavyo: Makleri, watawa wasio Makleri, walei, vijana na watoto. Yafuatayo ni maazimio/tamko la Hija na Kongamano la kilele cha mwaka wa IMANI:

4.1 Makleri:
    Kujenga uwezo wa makatekista na waalimu wa kujitolea ili waweze kutoa mafundisho ya Dini kwa makundi mbalimbali zikiwemo shule za msingi, sekondari na vyuo.
    Kuweka mikakati ya kuwajenga kiimani viongozi wakatoliki wa serikali na siasa ikiwemo kuanzisha “chaplaincy” bungeni Dodoma.
    Makleri kuwa karibu na waamini ili kuwasindikiza katika malengo yao ya kuishi Injili katika ulimwengu.
    Ekaristi ibaki kiini cha imani yetu.

4.2 WALEI
    Utengenezwe utaratibu mzuri wa malezi utakaowawezesha mapadri wapya kutekeleza wito wao kikamilifu.
    Kuweka msisitizo katika uanzishwaji wa shule za sekondari za wasichana na kuhakiksha wanapata maandalizi mazuri ya kuwa walezi wa familia.
    Katiba ya Halmashauri Walei iruhusu makundi yote ya Walei kushiriki kikamilifu katika kutoa maamuzi.
    Kutoa elimu na mafunzo kwa walei na makleri ili kujua majukumu na mipaka yao.
    Kuendelea kupata makongamano ya IMANI hasa vijijini.
    Kuweka shuhuda za matukio mbalimbali ya kiimani katika Kanisa Katoliki na kuona uwezekano wa kushughulikia mchakato wa kuwatangaza watakatifu wale waliotuletea Imani Katoliki.
    Kuweka utaratibu wa kupeana uzoefu Majimbo kati ya kwa Makleri.
    Kuwe na mkakati wa kuhuisha JNNK na ushiriki wa wanaume katika jumuiya.
    Kuhamasisha walei kugombea nafasi za uongozi wa kijamii kisiasa na serikali.
    Kitabu cha mafundisho ya Kanisa kuhusu jamii kichapishwe na kusambazwa.
    Tutumie Pro-life ili kupeleka UFATA maeneo ambayo haujafika.
    Elimu ya kukabiliana na athari za utandawazi itolewe kwa vijana.


4.3 WATOTO
    Kuwashawishi watoto wenzao kuingia kwenye Shirika ili watoto wamjue Yesu.
    Kuwa na upendo kwa watoto wenzao hasa wale wenye matatizo ili wadumu katika umisionari
    Kusaidia maskini na wagonjwa na pia kuwa na siku moja ya kutembelea yatima (watoto) wagonjwa n.k.
    Kutoa mrejesho wa kongamano kwa watoto wenzao kwa yale waliyoyapata.
    Wazazi wasiwakataze, bali wahamasishe watoto kuingia kwenye Utoto Mtakatifu.
    Watoto wafundishwe dini vizuri.


4.4 WATAWA
    Kutoa malezi endelevu kwa Watawa wote ili kuwaimarisha kiimani, kimaendeleo na kimtandao (mawasiliano)
    Kutoa huduma ya masakramenti na nafasi ya kuwasikiliza watu
    Watawa wapatiwe mahitaji muhimu, ikiwemo elimu, kutokanana na utume wao Parokiani/Taasisi za Jimbo n.k ili kuboresha utume kuendana na karama za shirika.
    Wakuu wa mashirika watume watawa wao katika utume kadiri ya uwezo.
    Mashirika ya kitawa yawe na mikataba na jimbo ili kuboresha utekelezaji wa utume kidini kuendana na karama za shirika na mazingira ya jimbo (inapowezekana kuwe na hati miliki za ardhi, mashamba n.k).
    Maparokiani mashirika ya kitawa na mapadre tuwe na utume pamoja ili kufanikisha kazi ya ufundishaji dini. Tuwe na vitendea kazi n.k.
    Tunahitaji kuimarisha Watawa katika kutoa huduma hasa huko Zanzibar ambapo ukristo unapingwa.


4.5 VIJANA:
    Kanisa litumie wataalamu wake wenye taaluma zao ili kupunguza gharama zake.
    Kanisa lazima litafute vitega uchumi vingine badala ya kutegemea sadaka na zaka pekee ili kutegemeza Kanisa.
    Kuwe na mafundisho endelevu baada ya Ekaristi Takatifu, kipaimara na ndoa kwa vijana.


HITIMISHO
Hija na Kongamano hili la Mwaka wa IMANI limetoa fursa ya kutimiza mwaliko wa Baba Benedikto wa XVI wa kujitathmini KIIMANI kama muumini mmoja mmoja na kama Kanisa linalosafiri. Limetoa mwelekeo wa tulikotoka, tulipo na tunapopaswa kuelekea katika IMANI yetu ya kikristo na hasa katika kukabiliana na changamoto zetu za sasa.

Ndugu zangu waamini wanafamilia ya Mungu, mwisho wa hija na kongamano hili ni mwanzo wa utekelezaji wa maazimio tuliyofikia leo ili tuwe chumvi yenye ladha na mwanga katika kukoleza maisha ya binadamu wa leo waweze kuonja matunda ya IMANI yetu.

Kwanza kabisa tunamshukuru Mwenyezi Mungu aliyetupa nafasi hii ya kuweza kuitafakari imani yetu.

Pili tunawashukuru waamini wote, walioshiriki kwa hali na mali, katika kufanikisha kongamano hili wakiwemo:-
    Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania na Wahashamu Maaskofu wote.
    Kamati mbalimbali za kongamano.
    Wakuu wa Mashirika ya Kitawa, ya kike na kiume.
    Taasisi mbalimbali za Kanisa vikiwemo Vyuo Vikuu na Seminari.
    Waamini wote.
    Jimbo Katoliki la Morogoro na namna ya pekee Mapadri wa Shirika la Roho Mtakatifu.
    Taasisi za Serikari na vyombo vya Usalama.
    Vyombo vya Habari na Wanakwaya.
    Wadau wote walioshiriki kwa namna mbalimbali wakiwemo wenye Mahoteli, vyombo vya Usafiri pamoja na Uongozi na wafanyakazi wote wa Stella Maris wakiwemo wapishi.



+ Tarcisius J.M. Ngalalekumtwa
RAIS WA TEC/ASKOFU JIMBO LA IRINGA


MUNGU AWABARIKI NYOTE!








All the contents on this site are copyrighted ©.