2013-11-15 12:34:36

Wakristo na Waislam wajitaabishe kufahamiana ili kujenga misingi ya haki, amani na utulivu kwa ajili ya mafao ya wengi!


Askofu mkuu Ignatius Ayau Kaigama, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria anawaalika Wakristo na Waislam kujenga utamaduni wa majadiliano ya kidini, kwa kujibidisha kufahamiana kwa dhati, ili kujenga misingi ya haki, amani na utulivu, wote kwa pamoja wakipania kutafuta mafao ya wengi. Juhudi hizi hazina budi kwenda sanjari na utamadunisho, ili kweli za Kiinjili ziweze kuingia katika maisha na vipaumbele vya waamini, ili Mkristo aweze kuwa kweli Mkristo na hapo hapo akiendelea kuwa ni Mwafrika pasi na mawaa!

Askofu mkuu Kaigama ameyasema hayo hivi karibuni wakati wa Maadhimisho ya Sinodi ya tatu ya Jimbo Katoliki la Enugu, nchini Nigeria. Haki msingi, utu na heshima ya binadamu ni mambo muhimu yanayopaswa kuwa msingi wa majadiliano ya kidini na kamwe watu wasikubali kugawanywa kwa misingi ya ukabila na udini.

Jamii za Kiafrika zijifunze kuenzi mila, desturi na tamaduni nzuri zinazopatikana kutoka katika makabila mbali mbali. Kwa Mwafrika wa kweli: ukarimu, upendo kwa maisha ya Kijumuiya, heshima kwa wazee ni mambo yanayopewa kipaumbele cha pekee. Mambo haya yakizingatiwa miongoni mwa Waafrika, kinzani, chuki, vita na uhasama wa kidini vitatoweka kama umande wa asubuhi.

Ingawa Nigeria ni kati ya nchi ambazo zinakabiliwa na tatizo la ukabila na udini, Askofu mkuu Kaigama anasema, bado wananchi wa Nigeria wanaweza kujikita katika mchakato wa majadiliano ya kidini na kiekuemene kwa ajili ya ustawi na mendeleo ya wengi; haki na amani. Ukosefu wa fursa za ajira miongoni mwa vijana, rushwa na ufisadi ni kati ya mambo ambayo yanawaandama wananchi lakini, wajanja wachache wanatumia migogoro ya kidini kwa ajili ya kukwepa uwajibikaji.

Licha ya majanga yanayoendelea kusababishwa na kikundi cha kigaidi cha Boko Haram, lakini bado Waislam na Wakristo wanaendelea kushirikiana kwa mambo mengi na kwamba, watu wachache wasiruhusiwe kuvuruga amani, utulivu na kiwango cha maendeleo kilichofikiwa!







All the contents on this site are copyrighted ©.