Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 33 ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa
Tunaendelea kama kawaida katika kipindi chetu, tafakari masomo Dominika, na leo tunatafakari
masomo Dominika ya 33 ya mwaka C wa Kanisa.
Tayari tunaelekea
kumaliza mwaka wa Kanisa, yaani tukiijongea Dominika ijayo iliyo Dominika ya mwisho
ambapo tutasherehekea Sikukuu ya Yesu Kristo Mfalme wa ulimwengu. Masomo yote matatu
yanachukua sehemu ya tafakari juu ya mwisho wa dunia, ambayo hasa ndiyo tabia ya Dominika
zote za mwisho wa mwaka wa Kanisa. Tabia hii kwa kifupi twaiona katika somo la pili
ambapo inaonekana katika jumuiya ya kwanza ya kikristu na hasa kati ya Wakristo wa
Thesalonike watu walianza kuacha kufanya kazi wakitarajia ujio wa pili wa Bwana kuwa
karibu.
Katika hilo Mtakatifu Paulo anawaonya akiwaambia yakuwa yampasa kila
mmoja kufanya kazi, uvivu unaojilaza katika subira ya ujio wa Bwana haukubariki. Katika
hili tunaweza kuona pia thamani ya kazi katika maisha ya mwanadamu. Kazi iwayo yote
iwe ya mikono au ya kiakili au ya kiroho ni ya maana mbele ya Mungu, aliyesema mkaitiishe
nchi.
Mpendwa msikilizaji, kama nilivyokwisha dokeza yakuwa masomo yetu, yatupa
hali itakavyokuwa wakati wa mapambazuko ya uzima wa milele, tunakutana na hali hiyo
katika lugha inayotisha na pengine yaweza kumfanya mtu aogope, na hasa katika ile
hali ya kutarajia maneno ya faraja na huruma. Hata hivyo hali hii ya kutisha ina
maana yake na baadaye itawekwa sawa na Mungu mwenyewe. Tunajua hilo kwa sababu kila
neno litokalo katika kinywa cha Mungu hata kama ni zito na kali lakini huwekewa mafuta
na kugeuka kuwa Neno na tangazo la matumaini kwa mpokeaji aliyeshiba imani!
Mpendwa
msikilizaji, kwa sababu hiyo basi yafaa kutenganisha kati ya maneno au lugha itumikayo
na ujumbe ambao Mungu apenda kutupatia. Lugha inayojitokeza katika masomo ya Dominika
za mwisho za mwaka ni lugha ya kiufunuo, lugha ambayo tunakutana nayo daima katika
kitabu cha Ufunuo. Ni wa namna hiyo basi kila mmoja wetu awe makini katika kupembua
ujumbe wa Neno la Mungu, asije akaangukia katika shimo la upotoshaji wa Habari Njema.
Mpendwa msikilizaji, tunasema hili kwa sababu ulimwengu wa leo ambao umejaa
fitina, ujangili pamoja na ughaidi unaweza kumfanya mtu badala ya kujenga matumaini
na kusonga mbele katika kutafuta amani, basi akaona hakuna haja kwa maana ni mikasa
tu ndiyo inayotuzunguka! Kuna baadhi ya wenzetu ambao pasipo kutafakari na kuchekesha
vema huibuka na mahubiri vitisho kuhusu mwisho wa dunia na huwajengea watu imani ogopeshi
ambayo haizaliwi toka upendo wa Kristu msalabani bali katika vionjo vya watu, imani
inayosisitiza hukumu badala ya upendo wa Mungu kwa wanadamu.
Mpendwa mwana
wa Mungu, tazama upendo wa Mungu pale msalabani, u-wazi anapomwambia yule mwizi tangu
leo utakuwa pamoja nami mbinguni! Bwana hapendi tumwogope bali tumpende, kwa maana
hakuna atakayepatilizwa kumbuka anasema “walakini hautapotea hata unywele mmoja wa
vichwa vyenu! Inatosha tu pasipo kuogopa kusubiri na katika subira hiyo basi tutaziponyesha
nafsi zetu. Upendo wa Mungu haurudi nyuma, jicho alilomtazama Zakayo ndilo hilohilo
jicho la milele ambalo atatutazama nasi katika nyakati za mwisho na sasa. Katika hii
basi Mungu anatudai kutumaini daima kama ambavyo yeye ni tumaini la kweli.
Kwa
nini jambo hili? Jambo hili linakuja katika tafakari kwa maana katika maisha yetu
kuna kishawishi kikubwa cha kuacha njia ya Bwana, njia nyembamba, njia ya maisha na
kufuata njia pana, njia ya kupoteza, njia ya kifo wakati wa taabu na shida katika
maisha yetu ya kila siku. Kumbukeni daima njia ya wokovu ni ndefu, ni siri ya Mungu
ambayo hufunuliwa kwa kila mmoja wetu katika tumaini la kweli. Ndiyo kusema nabii
Malaki anasema kwenu ninyi mnaolicha jina langu, jua la haki litawazukia lenye kuponya
katika mbawa zake. Kumbe siri ya Mungu tunaigundua katika kulicha jina lake na kutumaini
wokovu pasipo kusita.
Mpendwa mwana wa Mungu, wanaolicha jina la Mungu ni wale
ambao kila siku ya maisha yao hutekeleza nyajibu zao katika familia na mahali pa kazi
kwa upendo usiodai faida bali unaolala na kujisimika katika matumaini na upole wa
moyo. Katika kujenga tumaini basi ni rahisi yatakapojitokeza matukio ya kutisha tunayoyasikia
katika Injili, mwamini kusima na kusonga mbele katika subira pasipo woga na kulicha
jina la Bwana.
Hili lina maana ya kwamba tusihangaike kutafuta namna ya ajabu
ya kuishi ukristu wetu bali namna ya kawaida iliyojaa mapendo thamini kwa ndugu na
jirani kama alivyofanya Msamaria mwema. Tukitenda kile cha kawaida kama Mtakatifu
Thereza wa Mtoto Yesu, basi tutakuwa na uhakika wa kujipatia njia nyembamba hata katika
mateso tunayokumbana nayo kila siku ya maisha yetu.
Basi mpendwa, tunapoelekea
kufunga mwaka wa Kanisa tunaalikwa kuwa na kitu cha kuweka mbele ya Mungu kama tiketi
yetu ya kuonana naye, na hivi basi usisahau kabisa yakwamba tumaini lako na imani
yako tendaji inayojenga familia ya Mungu ndizo tiketi mwafaka kwa ajili ya sherehe
hiyo.
Mpendwa msikilizaji, Baba Mtakatifu Francisko katika barua yake ya Kitume
Mwanga wa Imani , anatufundisha kuwa mwanga wa imani unadai kuwekwa katika huduma
ya sheria ya haki, na amani, mwanga huo unakuwa ni uwezo unaoongeza nguvu katika mahusiano
ya binadamu, na katika kuboresha maisha ya pamoja na mshikamano wa kijamii. Imani
inafanya sisi kufahamu usanifu wa mahusiano kati ya binadamu kwa sababu imani huzingatia
msingi ya adilifu katika muono wa sheria za Mungu. Na hivyo imani inakuwa huduma kwa
manufaa ya wote.
Mpendwa, imani ni zawadi ambayo inadai kutunzwa pia ili
isipotee na haipaswi pia kutunzwa tu katika moyo wetu bali lazima ijitokeze nje ili
kuweza kushirikisha wengine tumaini la kweli na upendo wa Mungu kwa ajili ya wote.
Imani huimarisha wengine na hivi tukaweza sote kuwa tayari kuisubiria siku ya mwisho
kwa furaha.
Nikutakie furaha na tumaini la kweli katika Mungu Mkuu, mpaji wa
mapaji na zawadi zote za mbinguni. Tumsifu Yesu Kristo. Tafakari hii imeletwa kwako
na Pd Richard Tiganya, C.PP.S.