Mwaka wa Imani Jimboni Singida ulilenga kuimarisha utume na maisha ya Makatekista!
Katika kutekeleza tamko la Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI, kuwa mwaka 2013 ni
mwaka wa Imani, Jimbo Katoliki Singida pamoja na majimbo yote Tanzania walipokea mwito
huo kwa hamasa kubwa kwa nia ya kuhuisha imani kwa vitendo.
Maswali yakilenga
kwenye misingi yetu ya imani ili kuona kweli kama bado tumesimama imara au tunayumbayumba
hasa kutokana na kushambuliwa kwa imani, kukithiri kwa utandawazi, imani kuonekana
kama kitu binafsi, kutaka kumwondoa Mungu katikati ya matukio yetu ya maisha na maisha
kwa ujumla nk. Kutafakari maadui wakubwa wa imani na jinsi ya kukabiliana nao, kuhuisha
maisha ya Kikristo kwa kuyasoma tena na tena Maandiko Matakatifu, Nyaraka za Mtaguso
Mkuu wa pili wa Vatican, na Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki. Haya yote yakiwa ni
rejea katika kuuishi Mwaka wa Imani.
Mbali na kuadhimisha mwaka wa imani,
Jimbo Katoliki Singida liliuita mwaka huu kuwa ni mwaka wa Makatekista. Hii inatokana
na ukweli kwamba, Makatekista ni wasaidizi wakubwa wa mapadre katika kufundisha imani.
Hivyo ukawekwa mkakati wa kutambua utume wao katika jumuiya za waamini, yaani kuanzia
ngazi za Jumuiya, Vigango, Parokia na Jimbo.
Ili kuitikia wito huo kiparokia,
Maparoko wa Parokia za Chibumagwa (Pd. Mulokozi Deusdedit, C.PP.S) na Kintinku (Pd.
Moses Gwao) wakishirikiana na kamati tendaji na Halmashauri ya Walei wa parokia hizo
waliona ni vyema kufungua na kufunga mwaka huo kwa pamoja kama kuonesha ujirani mwema
kiimani.
Hivyo, tarehe 10/2/2013 Misa kubwa ya ufunguzi ilifanyika katika
Parokia ya Bikira Maria Mpalizwa-Chibumagwa ambapo waamini wa parokia zote mbili walishiriki
kwa kishindo kikubwa. Katika ibada hiyo Makatekista walirudia kiapo chao cha uaminifu
katika kufundisha imani ya kweli na kuendelea kuwa waaminifu katika uongozi wa Kanisa.
Walirudia ahadi zao kwa kusali Kanuni ya Imani wakiwa na mishumaa inayowaka kama ishara
ya uwepo wa Kristo shahidi mkuu na mwanzilishi wa imani yao. Vile vile watoto wapatao
sita walibatizwa. Misa hiyo iliongozwa na Pd. Mulokozi Deusdedit, akishirikiana na
Mapadre watanao na Mashemasi wawili.
Sasa, Parokia hizi mbili tayari wameanza
mchakato wa kufunga mwaka wa imani, kama walivyofungua pamoja wamekubaliana kwenye
kikao kuwa Misa ya kufunga itafanyika katika Parokia ya Kintinku tarehe 30/11/2013.
Ibada takatifu ya misa itaanza saa 3:00 asubuhi ikitanguliwa na maandamano yatakayoanza
saa 1:45 asubuhi. Mbali na mambo mengine dhamira kuu ni kuwaenzi Makatekista ambao
wamekuwa msitari wa mbele katika: kuikiri, kuifundisha, kuiishi kwa vitendo sanjari
na kuisali katika vigango vyao.
Katika ibada hiyo Makatekista 42, watatunukiwa
vyeti kama ishara ya kutambua mchango wao katika kuipokea, kuiishi, kuifundisha na
kuisali imani. Kati yao wapo Makatekista 3 ambao wameanza utume wao mwaka 1963.
Alama
ambazo zimechaguliwa kwenye vyeti vyao ni pamoja na Biblia na Msalaba. Bila kusahau
Nembo ya mwaka wa imani kuwa ni mtumbwi ambao wote tumo tukisafiri kwa pamoja kumwelekea
muasisi wa imani ambaye ni Kristo mwenyewe. Na kwa kuyakumbuka maneno ya Mtume Paulo
"Simameni imara katika imani yenu" (1Cor. 16:13), waamini wote watakumbushwa wajibu
walio nao katika kutunza imani ambayo thamani yake ni kubwa katika maisha yao.
Akiwakumbusha
umuhimu wa mwaka wa imani Baba Paroko wa Parokia ya Chibumagwa Pd. Mulokozi Deusdedit
alisema: mwaka wa imani ni tunu kwetu, kujifunza upya misingi ya mafundisho yetu ya
imani, tupokee wongofu mpya na wa kweli. tunaangalia imani kama mwenzi anayetusaidia
kutambua maajabu anayotenda Mungu. tunaalikwa kusoma, kutafakari, na kulimega Neno
la Mungu, kujiimarisha katika kulijua, ili tubidiishwe na kushibishwa nalo.
Imani
yetu itufanye tujibu upendo wa Mungu wa Yeye kujifunua kwetu. Imani itusaidie kujibu
swali la Nini maana ya maisha yetu. yaani kumjua, kumpenda, na kumtumikia Mungu na
mwisho kufika kwake mbinguni. Shughuli zetu za kuajiriwa katika nafasi mbalimbali
maofisini, biashara zetu, mashamba yetu, ufugaji wetu, je, vinatusaidia kujibu swali
hilo?
Imani ni kipawa kutoka kwa Mungu, ili kwa neema ya Mungu tupate kufikia
wongofu. Neno la Mungu linatakiwa kutupyaisha, kwa kulisikiliza kwa makini na kung'amua
kile ambacho Roho Mtakatifu analiambia Kanisa. Imani itusaidie kutambua thamani
ya tunu bora za kibinadamu kama vile: ndoa takatifu, kuthamini maisha na kuachana
na utamaduni wa kifo, kuacha kuaharibu mimba, madawa ya kulevya, nk. Imani inawataka
watu wawe na matamanio ya matashi halali kama vile kuyakemea kwa jina la Yesu yale
yote yanayotaka kuingiza mawazo au matendo ya jinsia moja.
Imani inatudai
uwajibikaji kuanzia kwenye familia, jumuiya, makazini, taifa kwa ujumla wake, Kanisa
kwa ujumla wake, kama anavyotufundisha Mtakatifu Yakobo kwenye barua yake kwa watu
wote. (2:14)"….kuna faida gani mtu kusema ana Imani lakini haoneshi kwa matendo."
Tuseme kaka au dada hana nguo, au chakula, yafaa kitu gani kuwaambia hao nendeni salama
mkaote moto na kushiba bila kuwapatia mahitaji yao ya maisha? Vivyo hivyo Imani peke
yake bila matendo imekufa kwa sababu haitazaa matunda. MWALIKO Waamini wote
wa Parokia za Kintinku na Chibumagwa pamoja na waamini wote, na watu wenye mapenzi
mema wanakaribishwa kwenye misa takatifu tarehe. 30/11/2013 katika parokia ya Kintinku
ili kumsifu Mungu na kujivunia imani yetu katika matendo. Imani yetu ni shirikishi.
Imani yetu ni hai na ni katika nafsi ya Yesu Kristo. WOTE MNAKARIBISHWA. Pd. Mulokozi
Deusdedit, C.PP.S. Paroko wa parokia ya Bikira Maria mpalizwa mBinguni - Chibumagwa Jimbo
Katoliki Singida. Tanzania.