Sekta ya kilimo, uvuvi na misitu imeharibika vibaya, uhakika na usalama wa chakula
uko mashakani!
Bwana Josè Graziano da Silva, Mkurugenzi mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja
wa Mataifa, FAO anasema, kiasi cha dolla za kimarekani millioni 24 zinahitajika ili
kuweza kukabiliana na maafa yaliyotokea nchini Ufilippini. Kiasi hiki cha fedha kinahitajika
ili kuweza kuwa na uhakika wa usalama wa chakula kwa waathirika hawa, kwani tufani
hii imesababisha uharibifu mkubwa katika sekta ya kilimo, uvuvi na misitu na kwamba,
watu wengi wamepoteza maisha yao.
FAO imeamua kuchangia kiasi cha dolla za
kimarekani millioni 1 na kwamba, itaendelea kuwahamasisha wadau mbali mbali kuchangia
kwa hali na mali, ili kuokoa maisha ya mamillioni ya watu walioathirika na tufani
ya Haiyan. Wakulima wengi nchini Ufilippini walikuwa wanajiandaa kwa ajili ya kuanza
kupanda mpunga mashambani mwao, juhudi zote hizi zimefutika kama ndoto ya mchana na
kwamba, mashamba mengi ya mpunga yameharibiwa vibaya kutokana na mafuriko. Miundo
mbinu ya barabara na mawasiliano bado ni mbaya kwa wakati huu.